Israel yatakiwa kulegeza vizuizi kupunguza njaa Gaza
3 Agosti 2025Wizara ya afya ya Gaza imesema Jumapili watu sita zaidi wamekufa katika saa 24 zilizopita kutokana na njaa na utapiamlo.
Vifo vya watu hao vimeongeza idadi ya waliofariki kwa sababu hizo na kufikia watu 175, ikiwa ni pamoja na watoto 93, tangu vita vya Gaza vilipoanza.
Wakati huo huo Shirika la habari la Al Qahera News lenye mafungamano na serikali ya Misri limeripoti kwamba malori mawili ya mafuta yaliyobeba tani 107 za dizeli yanatarajiwa kuingia Gaza siku ya Jumapili, miezi kadhaa baada ya Israel kuweka vizuizi vya kuingiza bidhaa na misaada mingine katika Ukanda wa Gaza.
Wizara ya afya ya Gaza inayosimamiwa na Hamas imesema uhaba wa mafuta unakwamisha uendeshaji wa shughuli mbalimbali katika hospitali.
Kuanzia mwezi Machi, uingizwaji wa mafuta na misaada mingine ndani ya Ukanda wa Gaza umekuwa nadra baada ya Israel kuweka vikwazo kama sehemu ya kuishinikiza Hamas kuwaachilia mateka waliobaki.
Israel inalaumu Hamas kwa mateso huko Gaza lakini, katika kukabiliana na malalamiko ya kimataifa yanayoongezeka, Israel, ilitangaza wiki iliyopita hatua ya kuruhusu misaada zaidi kuwafikia watu, ikiwa ni pamoja na kusitisha mapigano wa siku kwenye baadhi ya maeneo, kuidhinisha misaada kudondoshwa kutoka angani na imetangaza njia salama na ulinzi kwa misafara ya malori yanayobeba misaada.
Mashirika ya Umoja wa Mataifa yamesema vifurushi vya chakula vinavyodondoshwa havitoshi na kwamba Israeli lazima iruhusu misaada zaidi kwa njia ya ardhi ni na ifungue njia zaidi za kufikisha misaada katika Ukanda wa Gaza uliloharibiwa na vita na njaa imekuwa ikizidi kuongezeka.
Chanzo: RTRE