ICC yataka hati ya kuwakamata viongozi wawili wa Afghanistan
24 Januari 2025Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai Karim Khan, amesema anatafuta vibali vya kuwakamata viongozi wakuu wa Taliban nchini Afghanistan kuhusiana na unyanyasaji wa wanawake na kutenda uhalifu dhidi ya ubinadamu.
Soma Zaidi: Taliban yasema mashambulizi ya Pakistan yameua 46 Afghanistan
Karim Khan, amesema maafisa wa ICC wamethibisha kwamba viongozi hao wawili wa Afghanistan wanawajibika kwa jinai kwa kuwatesa wasichana na wanawake wa Afghanistan, na pia watu ambao Taliban inawaona kuwa hawakubaliani na matarajio ya itikadi zao katika swala zima la utambulisho wa jinsia au kujieleza.
Ameongeza kusema kuwa mateso hayo yalifanywa kuanzia kwenye tarehe 15 Agosti mwaka 2021 na yanaendelea kufanyika hadi hii leo katika maeneo yote ya Afghanistan na kwamba yanawakumba pia watu ambao Taliban wanawaona kuwa ni washirika wa wasichana na wanawake.
Naibu waziri wa mambo ya ndani wa Afghanistan Mohammad Nabi Omari, mfungwa wa zamani wa katika jela ya Guantanamo Bay, amesema nchi yake haitishiki na uamuzi wa ICC.
Akizungumza kwenye hafla iliyohudhuriwa na waandishi wa habarti wa shirika la Habari la AFP katika mji wa Khost ulio mashariki mwa Afghanistan amesema Mahakama ya ICC ilitakiwa kwanza kuifikisha Marekani mbele ya mahakama hiyo kwa kusababisha vita nchini Afghanistan.
Majaji wa ICC sasa watalizingatia ombi la Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Jinai Karim Khan kabla ya kuamua kutoa hati hizo za kukamatwa viongozi wawili wa Afghanistan. Mchakato huo unaweza kuchukua wiki au hata miezi kadhaa.
Soma Zaidi: Taliban yaiomba dunia kuisaidia
Mahakama ya ICC yenye makao yake makuu mjini The Hague, ilianzishwa ili kutoa uamuzi kuhusu matendo ya uhalifu kutoka kote duniani, kwa mfano uhalifu wa kivita na pia uhalifu dhidi ya binadamu.
Chanzo: AFP