Hamas yasisitiza makubaliano 'ya kina' kumaliza vita Gaza
7 Mei 2025Kauli hii inajiri huku taarifa za waokoaji zikisema kwamba mashambulizi ya Israel yamewauwa takribani watu 26 hivi leo.
Israel inadai kurejeshwa kwa mateka wote waliokamatwa katika shambulio la Hamas na kupokonywa silaha kwa Hamas, jambo ambalo kundi hilo limesema kamwe halitowezekana.
Soma pia: Israel yaidhinisha operesheni mpya ya kijeshi kuitwaa Gaza
Makubaliano ya usitishaji mapigano kwa miezi miwili katika vita hivyo yalisambaratika mwezi Machi, huku Israel ikirejelea mashambulizi makali na kuweka kizuizi kamili cha misaada kuingia katika eneo hilo la ardhi ya Palestina.
Mjumbe wa ofisi ya kisiasa ya Hamas, Bassem Naim, amesema wao na makundi mengine ya wanamgambo wanasisitiza kufikiwa makubaliano ya kina na mpango kamili wa kumaliza vita na uchokozi, na kuweka mpango wa siku zijazo, na kwamba kando ya hayo, hakuna haja ya kuendelea na majadiliano na Israel.