Finland yaunga mkono suluhisho la mataifa mawili
5 Septemba 2025Tamko hilo la Finland ni matokeo ya mkutano wa kimataifa uliofanyika mwezi Julai na ulioandaliwa na Saudi Arabia na Ufaransa, ambao ulisusiwa na Israel na mshirika wake mkuu, Marekani.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Finland Elina Valtonen ameandika kwenye ukurasa wa mtandao wa kijamii wa X kwamba, mchakato unaoongozwa na Ufaransa na Saudi Arabia ni mojawapo ya jitihada kubwa zaidi za kimataifa kuweka mazingira ya suluhisho la mataifa mawili.
Saudi Arabia na Ufaransa zimezihimiza nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa kuunga mkono tamko hilo, ambalo linatoa mwito wa "hatua dhahiri, zenye muda maalum na zisizoweza kurudishwa nyuma” kuelekea utekelezaji wa suluhisho la mataifa mawili.
Hata hivyo, tofauti na baadhi ya mataifa mengine ya Ulaya kama vile Uhispania na Norway, Finland haijaitambua Palestina kama taifa huru. Serikali ya muungano ya Finland imegawanyika kuhusu suala hilo.