Dunia yaadhimisha miaka 80 ya mwisho wa Vita Kuu ya Pili
8 Mei 2025Katika maadhimsho haya takriban viongozi 27 wa mataifa ya kigeni wanatarajiwa kuwasili nchini Urusi kwa ajili ya gwaride kuu la kijeshi la Siku ya Ushindi, hapo kesho Mei 9.
Maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 80 ya mwisho wa Vita vya Pili vya Ulimwengu barani Ulaya na kuanguka kwa udikteta wa Kinazi yalianza mjini Berlin hii leo kwa ibada kanisani, iliyohudhuriwa pia na Kansela mpya wa Ujerumani Friedrich Merz.
Rais wa Bunge la UjerumaniJulia Klöckner amesema, lazima taifa hilo pamoja na watu wake watambue "kiwango cha kutisha" cha uhalifu uliofanywa wakati wa Vita vya Pili vya Dunia. Aidha Klöckner amekumbushia wahanga waliosahaulika wa vita hivyo vya kikatili, ambavyo Ujerumani ilivianza kwa kuivamia Poland mnamo Septemba mwaka 1939.
Hapo awali, viongozi 29 walipanga kuhudhuria sherehe hizo mjini Moscow lakini marais wa Azerbaijan na Laos walijiondoa dakika za mwisho, kwa mujibu wa taarifa ya ikulu ya Urusi.
Soma pia: Ujerumani bado haina sikukuu rasmi ya Mei 8
Wageni waalikwa
Wageni muhimu zaidi kwenye gwaride hilo ni pamoja na Rais Xi Jinping wa China na Rais Luiz Inacio Lula da Silva wa Brazil.
Xi yupo Moscow kwa ziara ya kitaifa na atafanya mazungumzo na Putin kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wao wa "bila mipaka,” uliotiwa saini siku chache kabla ya Urusi kupeleka wanajeshi Ukraine.
Hapa nchini Ujerumani Rais wa Frank-Walter Steinmeier alikuwa na haya ya kusema "Hata kama hili litadaiwa tena kesho katika sherehe za ushindi huko Moscow, vita dhidi ya Ukraine si mwendelezo wa mapambano dhidi ya ufashisti."
"Vita vya uvamizi vya Putin, kampeni yake dhidi ya nchi huru ya kidemokrasia, havina uhusiano wowote na vita dhidi ya dhulma ya Wanazi katika Vita vya Pili vya Dunia."
Huku haya yakijiri rais wa China Xi Jinping alimwambia mwenzake wa Urusi Vladimir Putin mjini Moscow kwamba China iko tayari "bila kuyumbayumba" kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na Urusi.
Akitetea "ukweli wa kihistoria" kuhusu Vita vya Dunia vya pili, ambavyo kiongozi huyo wa Urusi anashutumu nchi za Magharibi kwa kutaka kupotosha, Putin amesema kwa pamoja na mshirika wake China watasisimama kidete kulinda ukweli wa kihistoria, kulinda kumbukumbu za matukio ya miaka ya vita na kukabiliana na maonyesho ya kisasa ya Unazi mamboleo na kijeshi.
Soma pia: Bomu la Vita vya Pili vya Dunia lagunduliwa Ufaransa
Viongozi wa Vietnam, Mongolia, Misri na Myanmar – wote ambao ni washirika wa muda mrefu wa Urusi – pia wanatarajiwa kuhudhuria, maadhimisho ya Mei 9, kwa mujibu wa Kremlin.
Kutoka Afrika, wakuu wa nchi za Burkina Faso, Zimbabwe, Jamhuri ya Kongo, Ethiopia na Guinea ya Ikweta pia watahudhuria.
Nchini Uigereza Mfalme Charles III alijiunga na maveterani na washiriki wengine wa familia ya kifalme kwa misa ya kuadhimisha kumbukukumbu hiyo mjini London.