Rais Xi Jinping akutana na waziri mkuu wa Uhispania
11 Aprili 2025Hivi sasa Rais Donald Trump wa Marekani ameifanya dunia kuwa roho juu kufuatia kishindo alichokianzisha cha kutangaza tozo kubwa za ushuru na wiki kisha wiki hii kutangaza siku tisini za kusitisha tozo hizo kwa nchi nyingi ili kutowa nafasi ya kufanyika mazungumzo.
Lakini China haimo miongoni mwa nchi zilizopewa fursa hiyo na badala yake imeongezewa ushuru wa jumla ya asilimia 145 na kitendo hicho kimeitanuwa vita ya kibiashara kati ya mataifa hayo mawili yenye uchumi mkubwa duniani.
Soma pia: EU kuweka shinikizo la kuondoa ushuru mpya wa TrumpKatika mazungumzo yake na waziri mkuu wa Uhispania leo Ijumaa mjini Beijing, rais wa China Xi Jinping, kwa mujibu wa shirika la habari la taifa, amesema kwamba China na Umoja wa Ulaya zinapaswa kuushirikiana kukabiliana na suala hilo la ushuru.
Waziri mkuu wa Uhispania Pedro Sanchez amemwambia rais huyo wa China kwamba nchi yake inataka kuona zaidi mahusiano yenye usawa kati ya Beijing na Brussels:
''Uhispania inapendelea zaidi kuona mahusiano yenye urari kati ya Umoja wa Ulaya na China, pamoja na kutafuta namna ya kupata suluhu kupitia mazungumzo kuondowa tofauti zetu, zilizopo na kuwa na ushirikiano mkubwa katika maeneo ambayo tuna maslahi ya pamoja.
Rais Xi Jinping ameisisitizia Umoja wa Ulaya kwamba inapaswa kutimiza wajibu wake wa Kimataifa na kushirikiana pamoja na nchi hiyo kupinga vitendo vya kibabe, akisema hatua hiyo sio tu italinda haki za kisheria na maslahi yao lakini pia italinda usawa na haki kimataifa.
Donald Trump ambaye amepania kuiendeleza vita ya kibiashara na China anasema anataka kupanga upya mwelekeo wa uchumi wa dunia kwa kuwalazimisha wenye viwanda kupeleka viwanda vyao Marekani na mataifa ya ulimwengu kuondowa vizingiti kwa bidhaa za Marekani.
Soma pia: Trump atishia ushuru zaidi kwa ChinaHata hivyo wanaomkosoa wanasema sera za kiongozi huyo zinasababisha mparaganyiko kwa makampuni ambayo yanategemea kupata bidhaa zao kutoka kwa wasambazaji wengi, na pia ni sera zinazowatenga washirika wa karibu wa Marekani na kufanya bidhaa kuwa ghali zaidi kwa wateja wa Marekani. Waziri mkuu wa Uhispania Pedro Sanchez akizungumzia zaidi vita hii ya kibiashara mjini Beijing alisema:
Nimemwambia rais Xi Jinping kama ambavyo nimewahi kusema kwa vyombo vya habari kwenye matukio mengine, kwamba vita ya kibiashara sio nzuri, hakuna mshindi kwenye vita hiyo na nina uhakika ulimwengu unazihitaji nchi zote mbili China na Marekani kukaa kwenye meza ya mazungumzo.''
China inapambana kutafuta washirika dhidi ya vita hivyo vya kibiashara vilivyoanzishwa na Trump,ambapo rais Xi Jinping wiki ijayo atakwenda Vietnam,Malysia na Cambodia ambako suala hilo la ushuru linatarajiwa kuchukuwa sehemu kubwa ya ajenda.