Brantner atoa wito wa vikwazo dhidi ya Smotrich na Ben-Gvir
11 Juni 2025Kiongozi huyo wa chama cha kijani nchini Ujerumani, amewashtumu mawaziri hao wawili kwa kuitisha wazi ghasia dhidi ya wakazi wa Palestina na kwa muda mrefu kueneza sera ya unyakuzi na uhamishaji.
Hatua ya Smotrich na Ben-Gvir yawatatiza wakazi wa Gaza
Brantner, ameliambia shirika la habari la dpa kwamba hatua hiyo inagharimu maisha ya wanadamu, kufanya jamii nzima kupoteza makazi na kusababisha vikwazo vikubwa katika njia ya mchakato wa amani.
Uingereza yawawekea vikwazo mawaziri wa Israel
Matamshi yake yanakuja baada ya Uingereza, Canada, Australia, New Zealand na Norway jana kutangaza kuwawekea vikwazo Ben-Givr, ambaye ni waziri wa ulinzi katika serikali ya waziri mkuu Benjamin Netanyahu na mwenzake wa fedha Smotrich.
Katika taarifa ya pamoja, mawaziri wa mambo ya nje wa nchi hizo tano
walimshutumu Smotrich na Ben-Gvir kwa kuchochea vurugu za itikadi kali na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu za Wapalestina.
Marekani yaikosoa Uingereza kuwafungia mawaziri wa Israel
Serikali ya Uingereza imesema kuwa vikwazo vya nchi yake vinahusisha marufuku ya usafiri pamoja na kufungia mali. Norway pia iliweka marufuku ya kusafiri .
Wakati huo huo, Marekani imeshtumu uamuzi wa Uingereza wa kuwaekea vikwazo mawaziri hao wawili.
Marekani yasema marufuku zarudisha nyuma juhudi za amani
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Marco Rubio, amesema kuwa marufuku ya kusafiri na kufungia mali iliyowekwa dhidi ya Ben-Gvir na Smotrich inarudisha nyuma juhudi zinazoongozwa na Marekanikufikia usitishaji wa mapigano na akatoa wito wa kubatilishwa kwa maamuzi hayo.
Kwa upande wake, waziri mkuu wa New Zealand Christopher Luxon, amesema ni muhimu kiishara kuonyesha kwamba wamekuwa na msimamo wa muda mrefu chini ya serikali mbali mbali kwamba makazi katika Ukingo wa Magharibi sio halali chini ya sheria za kimataifa.
Israel yawashambulia maelfu ya watu karibu na kambi ya msaada
Msemaji wa shirika la ulinzi wa kiraia la Gaza Mahmud Bassal , ameliambia shirika la habari la AFP kwamba wamesafirisha miili ya watu 31 na majeruhi 200 kutokana na shambulizi la droni laIsrael dhidi ya maelfu ya watu waliokuwa wanaeleka katika kambi ya msaada ya Marekani kupokea chakula. Hata hivyo jeshi la Israel halikujibu mara moja ombi la tamko kuhusu hali hiyo.